• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 9:15 PM
JAMVI: Mkanganyiko mkuu unaogubika siasa za urithi Pwani

JAMVI: Mkanganyiko mkuu unaogubika siasa za urithi Pwani

Na MOHAMED AHMED

KWA muda sasa magavana watatu kutoka Pwani akiwemo wa Mombasa Hassan Joho, Salim Mvurya wa Kwale na mwenzao wa Kilifi Amason Kingi wameonekana kuweka mipango yao ya kisiasa ambayo itakuja baada ya kumaliza hatamu zao.

Magavana hao wapo kwenye hatamu zao za mwisho kwenye viti hivyo ambavyo itakuwa wamevishikilia kwa muda wa miaka kumi wakati awamu zao zitakapokamilika mwaka 2022.

Wakati viongozi hao wanapopanga kuondoka kwenye nafasi hizo, tayari kuna wale ambao wanamezea mate viti hivyo na kutaka kuwarithi. Baadhi ya wanaomezea mate ni wale ambao magavana hao pia wangependelea wachukue nafasi hizo wakati watakapokuwa wameondoka.

Miongoni mwa viongozi ambao kufikia sasa wameonyesha azma ya kurithi viti hivyo ni pamoja na naibu gavana wa Kwale Fatuma Achani ambaye pia anaungwa mkono na Bw Mvurya

Mpinzani

Kufikia sasa mbunge wa Lunga Lunga Khatib Mwashetani ameonekana kuwa mpinzani wa karibu wa Bi Achani.

Licha ya Bw Mvurya kuwa chama kimoja cha Jubilee na Bw Mwashetani gavana huyo amesisitiza kwamba Bi Achani ndiye anastahili zaidi kumrithi ifikapo 2022

Katika mkutano wa hivi majuzi kwenye mazishi ya Askofu Morris Mwarandu Bw Mvurya alisema ni Bi Achani pekee atakayeweza kuendeleza mafanikio ambayo kaunti hiyo imeshuhudia tangu 2013

“Ni vile hapa ni mazishini sitaongea zaidi. Lakini Askofu aliniambia ‘muda wako unaisha ututayarishie ya mbele’. Naibu gavana ametayarishwa. Mnaona Tanzania hakujakuwa na msukosuko? Katika taasisi ni lazima watu watayarishwe,” akasema.?

Wengine wanaoaminika kumezea mate kiti hicho ni pamoja na aliyekuwa Mbunge wa Mtuga Chirau Mwakwere, na katibu wa Wizara ya Kilimo Hamadi Boga.? Mara kwa mara Bi Achani na Bw Mwashetani wamekuwa wakitoleana cheche za maneno ambazo zinaelekezwa na mipango yao ya kurithi Bw Mvurya

Cheche hizo za maneno ya kisiasa pia zimekuwa zikushuhudiwa katika kaunti ya Mombasa ambapo baadhi ya viongozi wanalenga kumrithi Gavana Joho.

Viongozi hao ni pamoja na Mbunge wa Mvita Abdulswamad Nassir, Mbunge wa Kisauni Ali Mbogo na mfanyabiashara Suleiman Shahbal ambao kufikia sasa ndio viongozi ambao wamejitosa ulingoni wazi wazi wakitaka kumrithi Bw Joho.? Hata hivyo, ukali wa siasa hizo za urithi zimeonekana kuelemea upande wa Bw Nassir na Bw Shahbal ambao ndio mahasimu wa karibu.

Huku Bw Nassir akionekana kusubiri kuidhinishwa na Bw Joho katika azma yake, Bw Shahbal ambaye pia sasa ana uhusiano wa karibu na Bw Joho amekuwa akiendeleza kampeni za mapema kupitia vikao vinavyotambulika kama “Gumzo Maskani”.

Kati ya mwezi wa Februari hadi mwezi jana, kiongozi huyo amefanya mikutano kadhaa katika maeneo bunge ya Mombasa ikiwemo Likoni, Changamwe, Mvita Kisauni na Jomvu kueleza sera zake.

Bw Nassir naye kwa upande amekuwa akitumia nafasi yake kama kiongozi kukutana na wakazi hususan wa eneo bunge lake la Mvita na kueneza azma yake ya kutaka kuwania ugavana.

Hata hivyo, Bw Nassir hajakuwa akionekana zaidi kwenye maeneo bunge mengine kufanya kampeni zake kama vile Bw Mbogo ambaye pia ameshikilia kampeni zake mashinani katika eneo bunge lake la Kisauni.

Uchanganuzi wa Jamvi umeonyesha katika miezi hiyo miwili iliyopita, Bw Nassir amezuru makanisa katika eneo la Changamwe mara tatu huku Bw Shahbal akitekeleza mikutano takriban 20 katika muda huo huo.

Kampeni hizo za mapema pia zimeibua tumbo joto katika chama cha ODM baada ya Bw Shahbal kutangaza kuwa anarudi kwenye chama hicho.

“Walinifungia mlango wakati ule wa nyumba lakini sasa si handisheki imekuja. Si tumerudi nyumbani?” Bw Shahbal alisema katika mmoja ya mikutano yake.? Tangazo hilo la Bw Shahbal lilipelekea Bw Nassir naye kumpiga vijembe mpinzani wake huyo na katika mkutano wa eneo la Jomvu akaonya wakazi dhidi ya kuchagua watu ambao ‘wanazuka saa hizi.’

“Mimi nataka kuwauliza wao walikuwa wapi wakati sisi tulikuwa tunapambana? Mimi nawaambia muwe makini na watu hao,” akasema Bw Nassir.? Licha ya wawili hao kujitokeza kumenyana kwenye kiti hicho, bado haijakuwa wazi iwapo Bw Joho atamuunga mkono yeyote kati yao.

Iwapo Bw Joho atajitokeza wazi kutaka kumuunga mkono kiongozi wa kumrithi basi naibu wake Dkt William Kingi atakuwa miongoni mwa wale wanaotarajia kuungwa mkono.

Dkt Kingi pia amewahi kutangaza kuwa atawania kiti cha ugavana, hata hivyo hakuna mikutano yoyote ya wazi ambayo ameanza kutekeleza.? Aliyekuwa seneta wa Mombasa Hassan Omar pia anatarajiwa kuwepo kwenye kinyang’anyiro hicho. Hata hivyo, bado pia yeye hajaanza kujitosa kwenye kampeni za mapema.

Kwa sasa, mwezi mtukufu wa Ramadhan utasitisha kampeni hizo kama ilivyo ada ya wanasiasa wa Mombasa huku kindumbwendumbwe kikitarajiwa baada ya mwezi huu ambao umeanza jana kukamilika.

Kwengineko katika kaunti ya Kilifi mihemko ya kisiasa ya kurithi Gavana Amason Kingi yamevutia aliyekuwa mbunge Gideon Mung’aro na mbunge wa Malindi Aisha Jumwa

Bado siasa hazijapamba moto eneo hilo lakini Bi Jumwa alikuwa ameonekana kuendesha siasa za chini kwa chini.

Bw Mung’aro naye ameonekana kuwa karibu na Bw Kingi ambaye kwa muda amekuwa akiendesha siasa za chama cha Pwani. Naibu gavana Gideon Saburi pia ametajika katika siasa hizo za urithi.

You can share this post!

JAMVI: Magavana ‘wanaofunga kazi’ wang’ang’aniwa na...

JAMVI: Miungano ya kisiasa inayobuniwa nchini ni ya kufaidi...