• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 6:50 PM
KINA CHA FIKRA: Asilan usikubali kushindwa hata kabla ya kujaribu

KINA CHA FIKRA: Asilan usikubali kushindwa hata kabla ya kujaribu

Na WALLAH BIN WALLAH

UNYONGE wa watu wengine ni kukata tamaa mapema hata kabla ya kujaribu kufanya shughuli au kazi fulani wanazopaswa kufanya!

Ni kasoro kubwa sana mtu kufikiria atashindwa kabla ya kupambana hadi mwisho!

Ni hatari kubwa kuanza kutoa vijisababu na visingizio vya hapa na pale kujitetea kuonyesha jinsi unavyodhania ungeshindwa kufanikiwa kuyatimiza malengo yako! Kwa kweli kushindwa kupo.

Kila mtu hutokea akashindwa! Lakini tabia ya kukata tamaa kabla ya kujaribu kupambana ni duni zaidi! Jaribu kwanza! Ukishindwa kila mtu atajua umejitahidi! Wewe pia utajua kuwa umejikakamua! Huko ndiko kushindwa kishujaa! Usikubali kushindwa kabla hujashindwa! Huo si ujasiri!

Duniani kuna mafanikio mengi! Lakini lazima yatafutwe! Yasipotafutwa hayawezi kupatikana kamwe! Tazama wadudu wadogo wadogo kama vile siafu, mchwa, vipepeo na nyuki wanavyojituma kusafiri kuenda mbali kuhemera ili wapate chakula na mahitaji yao mengine bila uzembe!

Aghalabu utawaona kwenye misafara na makundi yao wakiwa wamebeba mizigo ya vyakula bila kukata tamaa! Na wanaishi hivyo miaka yote! Kwani wadudu hao wana busara au akili gani kuliko baadhi yetu sisi wanadamu? Tusikubali kushindwa kabla ya kujaribu! Atafutaye hachoki; labda achoke akishapata!

Hebu tukumbushane kidogo! Wiki iliyopita matokeo ya mtihani wa darasa la nane yalitangazwa! Tuwapongeze zaidi wanafunzi waliofanya mtihani huo katika wakati mgumu wa janga la corona pamoja na walimu wao waandalizi! Pongezi kwenu nyote!

Licha ya matokeo mema yaliyopatikana, usidhani wanafunzi wote wa darasa la nane walifanya mtihani! La, hasha! Wengine walihepa na kujificha bila ya kufanya mtihani kwa vijisababu na visingizio mbalimbali! Wapo waliosingizia hali ngumu kutokana na corona wakiamini kwamba kufanya mtihani ni kuanguka tu! Wakaamua kushindwa hata kabla ya kujaribu! Wengine walisingizia ujauzito! Ati walichelea kuenda kwenye mtihani wakiwa wajawazito ilhali serikali ya nchi yetu iliwasihi na kuwarai wasikose mtihani kwa vyovyote vile! Wakashindwa kabla ya kujaribu!

Wanafunzi wengine waliamua kuacha kufanya mtihani kwa visingizio kwamba hata kama wangefaulu vizuri, wasingepata pesa za kulipia karo katika shule za sekondari! Na wengine waliamini mtihani ni mgumu tu kwa watu ambao hawakuenda shuleni miezi mingi! Nao wakashindwa hivyo bila kujaribu!

Ndugu wapenzi, jaribu kwanza. Usikubali kushindwa maishani kabla ya kujaribu!

You can share this post!

SAUTI YA MKEREKETWA: Heko tolatola kwa Baraza la Magavana...

Kocha Ryan Mason aaminiwa nafasi ya kushikilia mikoba ya...