• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 9:50 AM
CHOCHEO: Usimpe mpenzi wako sababu ya kukushuku

CHOCHEO: Usimpe mpenzi wako sababu ya kukushuku

Na BENSON MATHEKA

JEPHINA alimtaliki mumewe Sammy kwa sababu ya kumchunga.

Kwa mwanadada huyu, hakuweza kuishi na mwanamume asiyeweza kumwamini.

“Alikuwa akifuatilia mienendo yangu hata kazini. Alinifanya nikose marafiki kwa kuwa alishuku kila mmoja; wanaume na hata wanawake. Alikuwa mzigo katika maisha yangu kwa miaka saba, mzigo ambao niliamua kuutua,” asema Jephina na kuongeza kuwa tangu apate talaka kutoka kwa Sammy, anajihisi huru.

“Nilikuwa ninapata kila kitu kwake isipokuwa imani. Alikuwa ameninunulia gari lakini kwa sasa ninapanda matatu kwenda na kutoka kazini nikifahamu hakuna mtu wa kunichunga kama mbuzi,” asema mwanadada huyu.

Masaibu sawa yalimfanya Maina, 32, kutengana na mkewe wa miaka mitano. Maina anasema kwamba mkewe alikuwa akimchunga hata zaidi ya mbuzi.

“Sikuwa na uhuru wa kuzungumza na wanawake. Ilikuwa kualika balaa kuwa na marafiki wanawake katika mitandao ya kijamii. Ilikuwa ngori hadi nikaamua kanuke,” asema Maina kwa sheng.

Wanasaikolojia wanasema kwamba kuchunga mchumba kiwango kwamba hawezi kuwa na uhuru wake kunamsababishia mfadhaiko.

“Kuna wengi wanaovumilia hali hii na ni makosa. Wanafaa kujitokeza na kutafuta ushauri nasaha. Hii ndiyo hatua ya kwanza. Suluhu ikikosa kupatikana hasa pale anayekuchunga anapoanza kukudhulumu kimwili kwa kukupiga, unaweza kuomba talaka au mtengane,” asema Brian Simiyu, mwansaikolojia wa kituo cha Maisha Mema jijini Nairobi.

Maisha ya mapenzi ya muda mrefu ikiwemo ndoa, yanafaa kuwa ya kuaminiana na sio kushukiana.

“Mtu anayechunga mchumba wake huwa na mapungufu mengi ikiwa ni pamoja na kukosa kumwamini mtu wake. Uhusiano wa aina hii hauwezi kudumu na ukidumu anayechungwa huwa mtumwa wa anayemchunga,” aeleza mwanasaikojia huyu. Hata hivyo, anasema mtu hafai kumpa mwenzake sababu za kumshuku na kumchunga.

“Baadhi ya watu huwafanya wachumba wao washuku tabia zao. Kwa mfano, ikiwa amekupata katika hali ya kutatanisha na mtu wa jinsia tofauti au mienendo ya watu unaotangamana nao katika shughuli za kijamii na kibiashara ni ya kutiliwa shaka basi utakuwa umempatia sababu za kukushuku na kukuchunga,” asema.

Tabia nyingine zinazofanya mtu kuanza kumchunga mpenzi wake ni kumpunguzia au kumnyima haki zake za ndoa. Kulingana na Zipporah Kinama, mshauri wa masuala ya mapenzi, mwanamume atashuku mke anayemkazia uroda na kumchunguza kubaini iwapo ana mipango ya kando..

“Vile vile, mke atashuku mume anayebadilisha tabia na kuanza kuchelewa kufika nyumbani au hata kulala nje,” asema. Zipporah asema sababu nyingine ya watu kuanza kushuku na kuwapiga darubini wachumba wao ni uraibu wa mitandao na matumizi ya simu.

“Simu zimezua balaa sana. Mtu anapigiwa simu na kuondoka aliko mchumba wake kwenda kuipokea. Katika kufuatilia kujua aliyepiga simu, balaa inazuka na uhusiano kuvurugika. Ni sawa na wanaozama katika mitandao na kukatiza mawasiliano na wachumba wao nyumbani,” asema Kinama.

Mtaalamu huyu ashauri watu kutowapa wachumba wao sababu za kuwachunga na wanaowachunga wapenzi wao bila sababu kukoma akisema kufanya hivyo kunaua imani katika uhusiano.

“Usimpe mtu wako sababu ya kukuchunga na vilevile usimchunge mtu wako bila sababu ya kufanya hivyo. Wacha kumpigia simu kumuuliza aliko kila dakika iwapo amekufahamisha kwamba atachelewa kazini au kwenye mkutano wa chama. Watu wanafaa kukomaa, kuheshimiana na kuaminiana. Kuchunga mchumba wako kunayumbisha uhusiano,” asema.

Hata hivyo, Simiyu asema hakuna makosa kuchunga mtu wako kuhakikisha usalama wake.

“Kuna watu wanaowajali zaidi wachumba wao kiasi kwamba wataenda kuwachukua wanapochelewa kazini au kuwapigia simu kila wakati kujua hali yao waliko. Baadhi ya wanaopigiwa simu huwa hawafurahii tabia ya wenzao wakishuku wanawachunga lakini wanafaa kuwashukuru,” asema Simiyu na kuongeza kuwa wanaokasirishwa na wachumba wanaowachunga kwa usalama wao wanawapa sababu za kuwashuku.

You can share this post!

Kigogo Ibrahimovic sasa kuchezea AC Milan hadi atakapotimu...

FATAKI: Uwongo wa waume ni mwingi; ni jukumu lako kuujua na...