• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 1:14 PM
TAHARIRI: Stars ianze kusaka vipaji mashinani

TAHARIRI: Stars ianze kusaka vipaji mashinani

KITENGO CHA UHARIRI

KOCHA wa Harambee Stars Jacob ‘Ghost’ Mulee anafaa kuzama mashinani ili kuwatambua wachezaji chipukizi wenye talanta ambao wanaweza kusaidia timu hiyo kung’aa katika mechi za kimataifa.

Kung’aa kwa baadhi ya wachezaji wachanga ndani ya klabu zao na katika mechi zao za kwanza kwa Stars katika kipute cha Bara Afrika (AFCON) mwezi uliopita, kunaonyesha kwamba talanta hizi zikukuzwa kwa wingi, basi Kenya itakuwa mbabe wa soka sio tu ukanda wa Afrika Mashiriki bali bara zima.

Kati ya wachezaji chipukizi ambao wanazidi kung’aa ni kiungo wa Gor Mahia Benson Omala ambaye wikendi hii anaelekea Uswidi ili kujiunga na klabu ya Linkoping City inayoshiriki ligi ya divisheni ya pili ya nchi hiyo.

Omala ambaye alitamatisha mtihani wake wa kidato cha nne katika shule ya upili ya Kisumu Day akiwa na umri wa miaka 18 pekee, ni kilelezo kuwa wapo wachezaji wenye talanta za juu kutoka nje ya Nairobi.

Mwanadimba huyo japo bado hajachezea timu ya taifa Harambee Stars, alionyesha makali yake akiwa Western Stima msimu wa 2019/20 alikofunga mabao saba na pia kuwa mwanadimba mdogo zaidi kuwahi kutwaa tuzo ya mchezaji bora, akishinda tuzo hiyo Disemba 2019.

Tayari akiwa na umri huo mdogo, alichezea Gor mechi za Klabu Bingwa Afrika (CAF) na mechi za ligi na ufanisi huo sasa utamwezesha kucheza soka ya kulipwa Uswidi.

Kinda mwingine ambaye anaendelea kung’aa ni Henry Meja anayesakatia mabingwa wa zamani Tusker. Kabla ya michezo yote kusitishwa, mwanadimba huyo mwenye umri wa miaka 19 alikuwa ashafungia Wanamvinyo hao mabao 10 baada ya kusakata mechi 16.

Meja, ambaye ni mwanafunzi wa zamani wa Shule ya upili ya Kakamega, alisajiliwa na Tusker baada ya kung’aa katika makala ya pili ya mashindano ya Cleophas Malala Cup mnamo 2019.

Kati ya wachezaji chipukizi ambao wamedhihirisha vipaji vya juu baada ya kusajiliwa kutoka mashinani ni Ambrose Sifuna wa Sofapaka, Nicholas Omondi wa Gor Mahia, Dickson Raila wa Migori Youth na Tedian Esilaba kati ya wengine.

Ufanisi wa wachezaji chipukizi ambao walitoka mashinani tayari unaonyesha kwamba kuna talanta nyingi mashinani na kocha Mulee anafaa kuwatazama au kuwatuma maskauti wake ili wawatambue ndipo wajumuishwe Harambee Stars.

You can share this post!

KAMAU: Viongozi watahadhari wanapopanga kukwamilia mamlakani

AKILIMALI: Mfumo bora kufanikisha kilimo cha matikitimaji