Na GEOFFREY ANENE
TIMU ya GSU itamenyana na Port Douala nayo KPA ivaane na Nemostar katika mechi za nusu-fainali za kuorodheshwa nambari tano hadi nane nchini Tunisia, Jumapili.
Wakenya GSU na KPA walibanduliwa katika vita vya kuwania medali kwenye mashindano hayo ya Afrika ya voliboli ya wanaume siku ya Ijumaa baada ya GSU kulemewa na wenyeji Esperance kwa seti 3-0 za alama 25-12, 25-22, 25-9 nao KPA walisalimu amri ya Zamalek 3-1 (25-13, 22-25, 25-16, 25-13).
Douala kutoka Cameroon walipoteza 3-0 (25-23, 25-21, 25-18) mikononi mwa Kelibia (Tunisia) nao Nemostar wakanyamazishwa na Swehly (Libya) 3-0 (25-19, 25-14, 25-19) katika michuano mingine ya robo-fainali.
Jumapili pia itakuwa zamu ya mabingwa hao wa mwaka 1984, 1987, 2008, 2009 na 2012 Zamalek kulimana na Swehly katika nusu-fainali ya kwanza nao mabingwa wa mwaka 1994, 1998, 2000 na 2014 Esperance na Kelibia watapepetana katika nusu-fainali ya pili.
Nafasi nzuri Kelibia wamefika katika mashindano haya ni fainali mwaka 2003 na 2004 walipopigwa na Al Ahly kutoka Misri. Kelibia wameajiri mchezaji wa zamani wa GSU, Abiud Chirchir.
Washindi wa medali ya shaba mwaka 2005 GSU walikamilisha makala yaliyopita katika nafasi ya tano nao KPA wanashiriki kombe hili kwa mara ya kwanza kabisa.