• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 11:05 AM
Kilio serikali za kaunti zikikosa kulipa mishahara

Kilio serikali za kaunti zikikosa kulipa mishahara

Na WAANDISHI WETU

WAFANYAKAZI katika baadhi ya serikali za kaunti wanateseka baada ya kukosa mishahara kwa miezi kadhaa.

Wengi wamefurushwa katika nyumba za kukodisha na kuandamwa na mashirika ya kifedha kwa kukosa kulipa mikopo. Katika Kaunti ya Taita Taveta, wafanyakazi wapatao 3,000, wanakabiliwa na wakati mgumu baada ya mwajiri wao kutangaza kuwa mishahara yao itacheleweshwa kwa mara nyingine.

Hii ni kutokana na Wizara ya Fedha kuchelewesha pesa za serikali za kaunti. Wafanyakazi hao wamekaa bila kulipwa mishahara kwa miezi miwili tangu Februari.

“Fedha za mwisho zilizotolewa na Hazina ya Kitaifa zilikuwa za Januari huku serikali ya kaunti hiyo ikiwa imelipa mishahara hadi Februari 2021. Hata hivyo, tutalipa mishahara hiyo wakati fedha zitakapotolewa,” alisema katibu wa Kaunti, Liverson Mghendi, kupitia barua kwa wafanyakazi.

Baadhi yao walifichua kuwa wametakiwa na wamiliki wa nyumba wanazoishi kulipa kodi au wahame kwa sababu ya kukosa kulipa kodi mara kwa mara.

Katika Kaunti ya Migori, vilevile, wafanyakazi wanapitia hali ngumu huku benki zikikwamilia mishahara yao baada ya kaunti kuchelewa kulipa pesa inazowakata ili kulipa mikopo yao.

Taifa Leo imebaini kuwa walioathirika zaidi ni waajiriwa walio na akaunti katika benki za KCB na National Bank, ambazo zimezuilia mishahara yao tangu Machi baada ya idara ya Fedha kukosa kulipa mikopo.

“Tunakabiliwa na wakati mgumu kabisa, wafanyakazi wengi wanaoweka pesa KCB na National Bank hawajapokea mishahara yao kwa miezi miwili kwa sababu idara ya Fedha haijalipa mikopo. Serikali ya Kaunti hutoa tu mishahara kwa jumla ambayo imezuiliwa na benki hizo,” alisema afisa wa kaunti.

Wauguzi na maafisa wa kliniki walioshiriki migomo kati ya Januari na Machi nao bado hawajapokea malipo yao. Kwingineko katika Kaunti ya Murang’a, baadhi ya wafanyakazi wanaingia katika mwezi wa tano bila kulipwa mishahara. Hii ni baada ya benki kufutilia mbali muafaka wa malipo baina yazo na serikali ya kaunti hiyo baada ya miezi mitatu ya kukosa kulipa mikopo ya awali.

“Ni jambo la kuhuzunisha sana kwetu. Malipo ya mishahara yamekuwa na matatizo na wakati mwingine tumecheleweshewa hata kwa miezi minne. Hii ni sawa na mateso,” mfanyakazi mmoja wa kibarua alieleza Taifa Leo.

Ripoti za Lucy Mkanyika, Ian Byron na Mwangi Muiruri

You can share this post!

Msichana akiri kubadilisha vipimo vya mimba kuokoa...

Knut yasaka pesa za kuandaa kongamano la wajumbe