• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 9:15 PM
King’ang’i na wanahabari tisa waachiliwa baada ya kulala seli

King’ang’i na wanahabari tisa waachiliwa baada ya kulala seli

Na George Munene

MBUNGE wa Mbeere Kusini, Bw Geoffrey King’ang’i, pamoja na wanahabari tisa waliokamatwa Jumamosi katika eneo la Makima, Embu, waliachiliwa huru Jumatatu.

Bw King’ang’i na wanahabari hao walikamatwa na polisi waliokuwa wakifurusha wakazi katika ardhi inayozozaniwa. Maelfu ya watu waliachwa bila makao baada ya nyumba zao kubomolewa eneo hilo Jumamosi.

Bw King’ang’i na wanahabari hao walizuiliwa katika kituo cha polisi cha Matuu, Kaunti ya Machakos, hadi jana walipoachiliwa.

Maafisa wa polisi waliojihami kwa silaha walishika doria shughuli hiyo ya ubomoaji ikiendeshwa katika vijiji vya Ndunguni, Twanyonyi, Muthithu, Kituneni, Nunga na Mwanyani vilivyoko Mbeere Kusini.

Waliwalaumu wakazi kwa kuvamia ardhi ya ekari 66,000 ya Mamlaka ya Mito Tana na Athi (Tarda). Mtu mmoja alipigwa risasi na kujeruhiwa wakati wa kisa hicho.

Polisi walisema kwamba walikuwa wakitekeleza agizo la mahakama lililoruhusu Tarda kuwafurusha wakazi kutoka ardhi hiyo ili igawanywe.

Mnamo Februari 16, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tarda, Emilio Mugo, aliwapa wakazi ilani ya kuhama eneo hilo.

Kulingana na Tarda, ilani hiyo ilifuatia agizo la mahakama watu wahame ili ardhi hiyo igawanywe. Lakini wakazi wanasema kwamba wamekuwa wakiishi katika ardhi hiyo kwa miaka mingi na hawataondoka. Walidai kwamba watu wenye ushawishi wanataka kunyakua ardhi hiyo .

“Tunachukuliwa kuwa maskwota katika ardhi yetu. Hii haikubaliki,” alisema mkazi mmoja kwa jina Elizabeth Syombua.

Bw Kinga’ngi alidai kwamba watu matajiri wanataka kunyakua ardhi na kudhulumu masikini.

You can share this post!

Nyoro, Wamatangi walaumiana kuhu utafunaji wa pesa za corona

Wezi wa mifugo sasa wageukia teknolojia kuiba, kuhepa polisi