• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 6:55 PM
FAUSTINE NGILA: Tuwazime wafisadi iwapo tunataka teknolojia itufae

FAUSTINE NGILA: Tuwazime wafisadi iwapo tunataka teknolojia itufae

Na FAUSTINE NGILA

Inashangaza kuwa licha ya Kenya kupiga hatua kubwa katika maendeleo ya kiteknolojia, karatasi bado zinatumika katika sekta mbalimbali humu nchini.

Sekta za bima, uanasheria, ardhi na afya zimelemewa kabisa kuongeza kasi ya huduma kwani bado zinategema karatasi ambazo huharibu wasaa na hata kupandisha gharama ya huduma.

Utapata kuwa mteja amekuwa akilipia bima ya afya, lakini anapohitaji hela hizo kutibiwa, hospitali na kampuni za bima zinachukua miezi mine kutoa zile hela za malipo.

Mchakato mzima hutumia zaidi ya stakabadhi nane za karatasi lakini kwa kutumia teknolojia, hatua zote za gharama ya matibabu zinaweza kuchukua siku moja tu.

Kwa sasa tunaelewa kuwa kuendelea kukwamilia mifumo ya kikale, hasa katika uanasheria, kumechelewesha kuamiliwa kwa maelfu ya kesi, na hivyo kuwanyima wananchi haki yao ya kikatiba.

Na ingawa Tume ya Ardhi Nchini (NLC) Jumatatu ilitangaza kuhamisha michakato yote kuhusu umiliki wa ardhi kwa mfumo wa kidijitali, pengo kubwa linalowapa mafisadi msukumo wa kubadilisha stakabadhi lafaa kuzimwa.

Hongera kwa NLC kwa kukubali kuwa umefika wakati wa vipande vya ardhi nchini kuuzwa au kumilikiwa kupitia stakabadhi za kidijitali, lakini inafaa kutambua kuwa wakora pia wana uwezo wa kutumia teknolojia hiyo kunyakua mashamba.

Si mara moja ambapo kumeripotiwa wizi wa fedha za umma katika mfumo wa serikali wa malipo maarufu kama Ifmis, ambao ulipozinduliwa ulisemekana kuwa ungemaliza ufisadi.Kilichofuata ni kinyume chake.

Maafisa wa serikali walikuwa wanatoa nywila zao kwa watu wasioruhusiwa kuingia kwa mfumo huo na kufanikisha malipo ya huduma hewa.Wengine walitengenezea watu wa familia zao akaunti kufanikisha utoaji wa hela kupitia kampuni zao wakidai zimepewa zabuni na serikali.

Hivyo, katika mradi wowote ule wa teknolojia unaohusu hela au mali ya thamani kama ardhi, hulka ya watu walioajiriwa kuusimamia inafaa kuchunguzwa kwa makini.

Watu wenye ushawishi mkubwa wa kifedha wanaweza kutumia wale maafisa wa chini kupata chochote watakacho mle ndani, na kujaribu kutoboa siri kama hizo ni kama kujiitia mauti.

Hali ni sawa katika sekta ya uanasheria ambapo visa vya faili muhimu za kesi kutoweka kwa njia isiyoeleweka si vigeni.Inapojaribu kuhamia mitandaoni, Tume ya Huduma za Mahakamani (JSC) yafaa kujua kuwa kufaulu kwake kutategemea jinsi majaji na mahakimu wanajitolea kukabili ufisadi.

Nimejionea kuwa licha ya uwepo wa teknolojia zinazoweza kuzima ufisadi kabisa kama blockchain, maafisa wa serikali bado hawako tayari kukumbatia ubunifu huo kutokomeza wizi wa mali ya umma.

Kwa yakini, teknolojia pekee haiwezi kuzima maovu yanayoendelea katika mashirika ya kiserikali, tunahitaji kukemea ufisadi, la sivyo, kuunda mifumo ya kidijitali kutakuwa ni kurahisisha ufisadi.

Tunafaa kuona adhabu kali zikitolewa dhidi ya maafisa wenye uroho wa kumumunya mamilioni ya walipa ushuru ili kuhakikisha mtindo huo haufikii mifumo ya kiteknolojia inayorahisisha huduma.

You can share this post!

JSC yateua Martha Koome kuwa Jaji Mkuu

Wakenya wamwomboleza Philip Ochieng’