• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 AM
Murathe sasa apotosha bunge kuhusu wizi wa mabilioni ya corona

Murathe sasa apotosha bunge kuhusu wizi wa mabilioni ya corona

Na LEONARD ONYANGO

NAIBU mwenyekiti wa Jubilee David Murathe Alhamisi alijaribu kupotosha kamati ya Bunge inayochunguza sakata ya wizi wa mabilioni pesa katika Shirika la Kusambaza Dawa (KEMSA).

Hii ni baada ya Bw Murathe kudai kuwa kampuni ya Kilig Limited, ambayo ni moja ya zinazodaiwa kulipwa mabilioni ya sakata ya Kemsa, inamilikiwa na washirika wa Naibu Rais William Ruto.

Lakini alipoitwa baadaye na kamati hiyo, mmoja wa waanzilishi wa Kilig Limited, Wilbroad Gachoka alikanusha madai hayo ya Bw Murathe akisema: “Mimi sina uhusiano wa aina yoyote na Ruto.”

Bw Murathe aliwadhamini wasimamizi wa Kilig Limited na Entec wakati kampuni hizo zilipotuma maombi ya kandarasi kwa Kemsa. Baadaye Kilig Limited ilipata kandarasi ya Sh4 bilioni.

“Hatukuwa na mkataba wowote tuliotia saini na Kilig Limited, bali nilikubali kuwa mdhamini wake kirafiki kwa sababu tunajuana,” akasema Bw Murathe.

Naibu mwenyekiti huyo wa Jubilee na ambaye ni mwandani wa karibu wa Rais Uhuru Kenyatta, alidai amekuwa akiwasimamia watu wengi ambao wamekuwa wakiomba kandarasi, wakiwemo hata wabunge.

“Sijawahi kujihusisha katika biashara au shughuli za kampuni ya Kilig Limited au Entec. Vilevile, sikuwa na uwezo wa kushinikiza Kemsa kulipa kampuni hizo baada kusambaza vifaa vya matibabu ya corona.

“Mimi si Mkurugenzi wa Kilig. Sina mkataba wowote na Kemsa na wala sikuletea mamlaka hiyo kitu chochote. Nilisimamia kampuni hizo lakini sikunufaika na chochote na wala hatukuwa tumeafikiana wanilipe,” akajitetea Bw Murathe.

Stakabadhi za kiapo zilizowasilishwa mbele ya PIC zinaonyesha kuwa Bw Murathe aliacha kuwa mfadhili wa Kilig Limited mnamo Agosti 2020 baada ya Kemsa kufuatilia mbali barua ya makubaliano ya kandarasi.

Wiki iliyopita, Mbunge wa Wajir Mashariki Rashid Amin alisema kuwa ufichuzi kwamba Bw Murathe alikuwa na uhusiano na kampuni ya Kilig Limited ilikuwa ishara kwamba uchunguzi unaoendelea kuhusiana na sakata ya Kemsa imeanza kuzaa matunda.

You can share this post!

Msongamano wa wagonjwa wazidi hospitalini

Tangatanga wapinga vikali mswada wa BBI