• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 10:55 AM
GWIJI WA WIKI: Mhadhiri, mkalimani na mtafsiri anavyochangia kwa makuzi ya Kiswahili

GWIJI WA WIKI: Mhadhiri, mkalimani na mtafsiri anavyochangia kwa makuzi ya Kiswahili

Na WINNIE A ONYANDO

Lugha sio tu chombo cha mawasiliano bali ni malighafi na rasilimali ya jamii ambayo inapaswa kutumiwa kujikuza, kuhifadhi tamaduni zetu kama jamii na kujenga uzalendo wetu hasa tunaporejelea lugha ya Kiswahili.

Kila lugha ina hadhi, hakuna lugha bora kuliko nyingine. Lugha ya Kiswahili inalipa hasa kwa wale wanaoienzi na kuichukua kama lugha yenye hadhi na haiba ya kipeke.

Kiswahili kama lugha kinafaa kutumiwa katika taasisi zote nchini Kenya kama njia mojawapo ya kuwasiliana hasa katika utoaji wa huduma katika ofisi zote za kiserikali.

Lugha ya Kiswahili inafaa kutumiwa nchini Kenya katika vikao vyote. Kila mwajiriwa katika ofisi, kampuni ama taasisi yoyote nchini Kenya anapaswa kutumia lugha ya hiyo kwa uweledi hasa katika utoaji wa huduma kwa umma.

Hayo ndiyo kauli na maoni ya Mhadhiri, Mtafsiri na Mkalimani wa lugha ya Kiingereza, Kiswahili na Kikuyu Bw Vincent Njeru Magugu.

Bw Magugu, 35 ni mpenda lugha aliyebobea katika taaluma ya Tafsiri. Yeye ni mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Moi (Bewa Kuu) mjini Eldoret anakofunza kozi la Kiswahili hasa Tafsiri.

MAISHA YAKE YA AWALI

Bw Magugu alizaliwa na kulelewa katika kijiji cha Marmanet, eneo la Nyahururu kaunti ya Laikipia, kitindamimba katika familia ya watoto watano.

Anaeleza kuwa japo wengi huchukulia kuwa vitindamimba hudekezwa na wazaziwe, yeye hakudekezwa na wazazi. Alitarajiwa kufanya vizuri shuleni jinsi wenzake walivyohitimu, wazazi wake pia walimtia adabu na kumhimiza atie bidi masomoni.

Wazazi wake marehemu Bw James Magugu na Bi Rose Wamucii ndio kielelezo wa kwanza maishani. Wamekuwa wakimhimiza aendelee kutia bidii masomoni. Mhadhiri huyo anaeleza kuwa ana mke na mtoto mmoja mvulana.

MASOMO

Mhadhiri huyo amaeleza kuwa alianza masomo yake katika shule ya Msingi ya kiserikali ya Kundarilla eneo la Nyahururu, alikosoma hadi darasa la saba na baadaye kuhamishwa katika shule ya Msingi ya kibinafsi ya Amazing Grace eneo la Nyahururu alikomaliza masomo yake ya shule ya Msingi.

Baada ya kukamilisha masomo yake ya Shule ya Msingi, alijiunga na shule ya Sekondari ya Wavulana ya Kanjuri, Nyeri.

Anaeleza kuwa japo alikuwa mwanafunzi wa wastani masomoni, alipata mwamko na msisimko mpya masomoni hasa baada ya kukutana na mwalimu wake wa Kiswahili Bi Lucy Mugo. Anaeleza kuwa Bi Mugo hakuchoka kumfuatilia na kumpa mawaidha kila uchao jinsi ya kujiimarisha masomoni na kuwa mwanafunzi bora.

Anaeleza kuwa kupitia mwalimu wake huyo, aliweza kupata alama ya A katika somo la Kiswahili na hata kupasi mtihani wake wa KCSE kijumla.

Magugu anasema kuwa ndoto yake ya kuwa Mwanasheria yalikatizwa baada ya rafiki yake waliyesoma naye pamoja katika shule ya Sekondari Harrison Ngure kumshawishi achague kozi ya Ba Kiswahili.

Hakuchelewa ila akachagua kozi hiyo katika Chuo Kikuu cha Moi (Bewa Kuu) Eldoret. Alijiunga na Chuo hicho mwaka wa 2007.

Chuoni Moi, aliweza kukutana na Prof Nathan Ogechi Mkuu wa Idara ya Kiswahili na Lugha Nyingine za Kiafrika ambaye alimpa ujasiri na kujenga imani yake kuwa BA Kiswahili kinalipa.

Kukutana kwake na hayati Prof Naomi Shitemi ilikuwa nyota la heri kwake. Prof Shitemi alimpa mawaidha kila mara kuhusiana na taaluma ya Tafsiri.

Anaeleza kuwa kwa wakati huo, walikuwa wanafunzi 12 waliojisajili kufanya kozi ya BA Kiswahili. Haya hayakumtia shaka kwa kuwa aliunyakua nafasi huo adimu ili kujiboresha katika lugha ya Kiswahili.

Wakati huo, yeye pamoja na rafiki yake Osinya Okumu walihimizana kila wakati na kudurusu somo la Kiswahili huku wakifanya mazoezi kila mara katika lugha ya Kiswahili.

Kuungana na Chama cha CHAKIMO akiwa katika mwaka wake wa Pili kilimfanya abobee zaidi katika lugha hiyo.

Wakati huo Bw Chris Adungo ndiye aliyekuwa mwenyekiti wa chama cha CHAKIMO Moi naye akachaguliwa Naibu mwenyekiti wa chama hicho mwaka wa 2008.

Chris alipomaliza masomo yake, Bw Magugu alichaguliwa mwenyekiti wa chama hicho. Amekuwa mwenyekiti wa chama hicho akiwa mwaka wa pili hadi mwaka wa tatu.

Baadaye alikuwa mhariri wa chama hicho ampabo walijiendeleza sana kama chama.

Baada ya kuhitimu Shahada ya Digrii, aliendelea na masomo yake ya Uzamili katika Chuo Kikuu cha Moi mwaka wa 2011 ambapo alikuwa mwanafunzi mmoja anayeandaa tasnifu ya Tafsiri. Alisaidiwa na Prof Shitemi na hatimaye kufuzu.

MAENDELEO TANGU AFUZU SHADADA YA UZAMILI

Baada ya kumaliza masomo yake ya Uzamili, alijiunga na Elgon View College ambapo aliajiriwa kama mwalimu. Alifunza somo la Kiswahili, Isimu na Tafsiri kwa muda mchache.

Baadaye, mwaka wa 2013, Chuo cha Moi kilitangaza nafasi ya ajira. Alipeleka barua zake za kuomba kazi na hatimaye akawa mhadhiri Chuoni Moi kuanzia mwaka wa 2014, Januari hadi sasa.

Aliweza kutafsiri kazi nyingi ikiwemo Mradi wa Chuo Kikuu cha Moi ‘Child Health Impact Studies,’ kazi ya Kitivo cha Afya kilichosimamiwa na Prof Omar Egesa.

Kazi nyingine alizotafsiri ni Mradi wa Bunge ya EACC alipotafsiri Kanuni za Kudumu za bunge. Ameweza pia kutafsiri kazi ya mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Moi Dkt Odiwuori ya ‘Asali Chungu’.

Ameweza pia kutafsiri kazi za wateja. Yeye hupata wateja kutoka nchi mbalimbali. Anasema kuwa kujenga ukuruba na wateja wako na hata kuwafanyia kazi nzuri kwa wakati ufaao ndiyo imekuwa ikimpa wateja wengi.

Mhadhiri huyo ameweza kuwasilisha namna ambavyo DJ Afro anatumia sauti mpachiko katika kuwasilisha kazi zake za video.

Magugu ameweza kutoa wanafunzi waliobobea sana katika tafsiri. Wengi wa wanafunzi wake wanafanya katika mashirika tajika nchini.

Sasa hivi, mhadhiri huyo ameanzisha program ya kutoa mafunzo ya tafsiri ambapo anawaelekeza na kuwashauri watafsiri wachanga Afrika.

Program hiyo ya Mentoring African Traslators umeanzishwa ili kuwakuza watafsiri na kuwapanua akili kiakademia katika taaluma ya tafsiri.

MCHANGO WAKE KATIKA CHAMA CHA CHAKIMO

Bwa Magugu anasema kuwa tangu ajiunge na chama cha Chakimo mwaka wa 2007, waliweza kufanikisha mengi.

Yeye pamoja na wenzake, kama vile Paul Ng’ang’a ambaye alikuwa mhariri wa chama hicho mwaka huo waliweza kuandaa michezo ya kuigiza ya vitabu vya fasihi ya Kifo Kisimani na Utengano. Mwaka wa 2009, alichaguliwa Katibu wa chama cha CHAWAKAMA Kenya.

Mwaka wa 2009 pia alichaguliwa kama Mhazini wa Afrika Mashariki. Waliweza pia kushirikiana na vyama vingene vya Kiswahili kutoka Vyuo vingine na kuandaa kongamano katika Chuo Kikuu cha Nairobi na Uganda.

Wakati wa masomo yake ya Uzamifu, alichaguliwa Kaimu Mlezi wa chama hicho. Hadi sasa Magugu ndiye mwenyekiti wa Taasisi ya Watafsiri na Wakalimani ya muungano wa EATIA.

CHANGAMOTO

Changamoto yaliyomkumba mhadhiri huyo hasa wakati wa masomo yake Chuoni ni ukosefu wa marejeleo ya kutosha. Baadhi ya vitabu vya marejeleo vimeandikwa katika lugha ya Kiingereza. Wakati wa masomo ya Uzamili na Uzamifu, alilazimishwa kutafsiri baadhi ya kazi hizo katika lugha ya Kiswahili.

Anaeleza pia kuwa, katika taaluma yake ya Tafsiri kutoka katika lugha ya Kiswahili, Kiingereza na Kikuyu, vitabu vya marejeleo ni chache sana hasa katika lugha ya Kikuyu. Analazimishwa kutafuta maneno mbadala yanayokaribiana kimaana na lugha lengwa.

Wasomi wengi pia hawajajitokeza kujifunza lugha ya Kiswahili. Wengi katika uzamili na uzamifu wanazamia Fasihi, Isimu na lugha huku wakitupilia mbali taaluma ya Tafsiri wakisema kuwa ni ngmu.

KICHOCHEO

Kilichomchochea mwalimu huyo kuzamia taaluma ya Tafsiri ni mengi sana. Mhadhiri wake marehemu Bi Shitemi alisimama naye na kumwelekeza kila akihitaji mawaidha na maelekezo katika taaluma ya tafsiri.

Wahadhiri wa tafsiri hawakuwa wenge wakati huo, Prof Shitemi na Dkt Odiwuori ndio walikuwa wamezamia sana taaluma ya tafsiri, aliunyakua nafasi huo na kuifanya kuwa kichocheo chake katika kuzamia taaluma hiyo.

Katika darasa lao, walikuwa wanafunzi 12 waliojisajili kufanya kozo ya BA Kiswahili. Hii ilimpa motisha na kumfanya atie bidi katika masomo yake.

Japo alikuwa mwanafunzi wa pekee aliyezamia Tafsiri katika Uzamili na hata Uzamifu, hakutiwa wasiwasi bali aliuchukua kama daraja la kuvuka katika kufikia upande wa mafanikio yake maishani.

Kila moja anaweza kufanikiwa katika daraja lolote maishani, ukakamavu, bidii na kumweka Mungu mbele ndiyo chanzo cha mafanikio maishani.

You can share this post!

Loroupe ataka viatu vya utata vya Kipchoge vipigwe marufuku...

Mashabiki 500 wa klabu za ugenini kuhudhuria mechi