• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 5:54 PM
Kaunti yapewa siku 7 kujibu kesi ya wafanyabiashara

Kaunti yapewa siku 7 kujibu kesi ya wafanyabiashara

Na PHILIP MUYANGA

SERIKALI ya Kaunti ya Mombasa imepewa siku saba kujibu kesi iliyowasilishwa kortini na chama cha wenye mabaa, hoteli na nyumba za wageni, kinachopinga Sheria ya Fedha ya Kaunti ya Mombasa 2021.

Jaji Eric Ogola wa mahakama kuu mjini Mombasa pia aliagiza chama hicho kuweka hati ya kiapo ya ziada iwapo wanahitaji wakati watakapopewa majibu na serikali ya kaunti.

Takriban wiki tatu zilizopita, mahakama kuu ilizuia kwa muda serikali ya kaunti kulipisha kodi au fedha za adhabu za mwaka jana kama kigezo cha kuruhusu wafanyibiashara kulipia pesa za leseni za mwaka huu.

Wafanyibiashara hao katika stakabadhi za kesi wanasema kuwa serikali ya Kaunti ya Mombasa inawalazimisha kulipa pesa za kodi na adhabu zingine za mwaka jana kabla ya kupewa leseni za kufanyia kazi za mwaka wa 2021.

Chama hicho kinasema kuwa serikali ya Kaunti imepuuza suala la kuwa serikali ya kitaifa ilikuwa imeagiza kufungwa kwa biashara mwaka jana kwa sababu ya ugonjwa wa Covid 19 na kwamba kuna biashara ambazo bado hazijafunguliwa hadi sasa.

Wafanyibiashara hao ambao wamewasilisha kesi pamoja na shirika la Coast Legal Aid and Resource Foundation (Clarf), wameshtaki serikali ya kaunti ya Mombasa, katibu wa bunge la kaunti ya Mombasa na wizara ya fedha ya kaunti.Kulingana na walalamishi, umma haukuhamasishwa kuhusu sheria hiyo ya fedha ilipoundwa.

“Washtakiwa waliwanyima wakazi wa Mombasa fursa ya kuhusika katika mchakato wa kutunga sheria hiyo ya fedha,” walisema.

Wanataka mahakama kuamua kuwa hatua za washtakiwa zilikiuka haki zao na katiba kwa kuwa hakukuwa na uhamasishaji wa umma wakati wa mchakato wa kutunga sheria hiyo.

Chama hicho na shirika la Clarf wanataka mahakama kuamua ya kuwa kitendo cha serikali ya kaunti cha kuwafanya walipe kodi na pesa zingine za mwaka jana kabla ya kupokea malipo na kutoa leseni ni kinyume cha sheria.

Pia wanailaumu serikali ya kaunti kwa kuongeza malipo na kodi inayowaathiri wao pamoja na wananchi bila kufuata sheria.Wanaongeza kusema kuwa sheria hiyo ya fedha iliongeza kodi ya vitanda katika hoteli ambayo italipwa kwa serikali ya kaunti licha ya kuwa malipo ya asilimia mbili katika Hazina ya Utalii huwa tayari imeshughulikia ada hiyo. Kesi itasikizwa Mei 27 mwaka huu.

You can share this post!

Tuungane tulinde maslahi ya Mlima Kenya – Kiunjuri

JUMA NAMLOLA: Marufuku yasitumike kuumiza mwananchi wa chini