• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 5:23 PM
Shule za kibinafsi zalalamikia ubaguzi

Shule za kibinafsi zalalamikia ubaguzi

Na WANDERI KAMAU

CHAMA cha Wamiliki wa Shule za Kibinafsi nchini (KPSA) kimelalamika kuwa wanafunzi katika shule hizo walibaguliwa kwenye zoezi la kusahihisha Mtihani wa Darasa la Nane (KCPE) mwaka uliopita.

Chama hicho kilisema uchunguzi wake umebaini kulikuwa na ubaguzi mkubwa kwenye matokeo hayo, kwa kuwa, yalitofautiana sana na utaratibu ambao kimekuwa kikitumia kutabiri matokeo hayo katika miaka ya awali.

Kwenye kikao na wanahabari jijini Nairobi jana, mwenyekiti wa chama hicho, Bw Steve Odero, alisema wanahofia huenda mapendeleo hayo yakajitokeza tena kwenye mchakato wa kuwateua wanafunzi watakaojiunga na Kidato cha Kwanza baadaye mwezi huu.

Bw Odero alisema ni makosa kwa Waziri wa Elimu, Prof George Magoha, kuwatofautisha wanafunzi wa shule hizo na zile za kibinafsi, akisema hilo linajenga taswira isiyofaa miongoni mwao.

“Ni wazi kulikuwa na mapendeleo makubwa kwenye utoaji wa matokeo ya mtihani wa KCPE mwaka uliopita. Kwa miaka mingi, tumekuwa tukitumia utaratibu maalum kubashiri vile wanafunzi wetu watakavyofanya mitihani yao ya kitaifa. Hata hivyo, hali ilikuwa kinyume mwaka huu, kwani utabiri wetu ulitofautiana kabisa na matokeo yaliyotolewa. Tunahofia huenda ubaguzi huo ukaendelezwa hata katika Mtihani wa Kidato cha Nne (KCSE),” akasema.

Kwenye matokeo ya KCPE mwaka uliopita, wanafunzi wa shule za umma walifanya vyema ikilinganishwa na wenzao katika shule za kibinafsi, hali ambayo imeendelea kuzua hisia miongoni mwa wadau wa elimu. Kwa mfano, miongoni mwa wanafunzi 15 bora nchini, kumi kati yao walitoka katika shule za umma, huku shule za kibinafsi zikiwa na wanafunzi watano pekee.

Taswira hiyo ni kinyume na miaka ya awali, ambapo shule za kibinafsi zimekuwa zikishikilia nafasi bora kitaifa, ikilinganishwa na wenzao katika shule za umma.

Ili kuhakikisha matakwa yake yanashughulikiwa ifaavyo, chama kililishinikiza Baraza la Kitaifa la Mitihani Kenya (KNUT) kuwajumuisha wawakilishi wake kwenye bodi yake. Bw Odero alisema ni hatua hiyo pekee itakayohakikisha wana usemi wa kutosha katika masuala yanayohusu uendeshaji na usimamizi wa mitihani.

You can share this post!

Mwingereza ataka jaji ajiondoe kwenye kesi ya ulezi wa mtoto

IG aunda kikosi kuchunguza mauaji ya wanne