• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 6:55 AM
Messi afunga mabao mawili na kuongoza Barcelona kucharaza Valencia 3-2 kwenye La Liga

Messi afunga mabao mawili na kuongoza Barcelona kucharaza Valencia 3-2 kwenye La Liga

Na MASHIRIKA

LIONEL Messi alifunga mabao mawili na kupoteza penalti katika gozi la Ligi Kuu ya Uhispania (La Liga) lililowashuhudia waajiri wake Barcelona wakitoka nyuma na kuwakung’uta Valencia 3-2 mnamo Jumapili usiku.

Ushindi huo uliwezesha Barcelona kuendeleza presha zaidi dhidi ya Atletico Madrid ambao kwa sasa wanadhibiti kilele cha jedwali la La Liga kwa alama 76. Barcelona wanakamata nafasi ya tatu kwa pointi 74 sawa na mabingwa watetezi Real Madrid.

Licha ya kwamba wana idadi ndogo ya mabao kuliko Barcelona, Real wameorodheshwa mbele kwa kuwa walishinda michuano yote miwili ya El Clasico msimu huu.

Sevilla ambao wana mchuano mmoja zaidi wa kusakata ili kufikia idadi ya mechi ambazo zimetandazwa na vikosi vitatu vya kwanza jedwalini, wanashikilia nafasi ya nne kwa pointi 70.

Beki wa zamani wa Arsenal, Gabriel Paulista, aliwaweka Valencia kifua mbele katika dakika ya 50 kabla ya Messi kusawazisha dakika saba baadaye kupitia mpira uliomrudia baada ya kukosa kufunga penalti.

Antoine Griezmann aliwaweka Barcelona uongozini katika dakika ya 63 kabla ya Messi kufunga bao lake la pili kwenye mchuano huo dakika sita baadaye. Carlos Soler alipachika wavuni goli la pili la Valencia kunako dakika ya 83.

Chini ya kocha Ronald Koeman, Barcelona wameratibiwa kupepetana na Atletico mnamo Mei 8, 2021 ugani Camp Nou katika mchuano ambao huenda ukaamua mshindi wa taji la La Liga muhula huu.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Bale ashiba sifa za kocha Mason baada ya kufungia Spurs...

Arsenal wacharaza Newcastle United 2-0 katika EPL