• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
CHOCHEO: Asali sio leseni ya ndoa

CHOCHEO: Asali sio leseni ya ndoa

Na BENSON MATHEKA

UHUSIANO wa Maria na Mike ulikuwa mzuri kwa miaka minne.

Maria alikuwa amekata kauli kwamba kapata mpenzi wa maisha yake. Wote wawili walikuwa viongozi wa vijana kanisani na Maria alikuwa amemweleza Mike kwamba hangeonja asali hadi watakapooana.

Ingawa Mike alijaribu mara kadhaa kumshawishi mwanadada huyu kumfungulia mzinga, alikataa na kumweleza aharakishe wafunge pingu za maisha ili waweze kufurahia tendo la ndoa wakiwa mtu na mkewe.

Mike alikubaliana naye na Maria akawa anasubiri waanze mipango ya harusi hadi juzi aliposhtuka kugundua kuwa aliyedhani kuwa mpenzi wa maisha yake alikuwa ameoa mwanadada mwingine.

“Ulikataa kunifungulia mzinga kabla ya ndoa, nikamuoa aliyekubali kunionjesha kwanza. Wewe endelea kusubiri atakayekubali muoane ili aweze kujua utamu wa asali iliyo kwenye mzinga wako,” Mike alimweleza Maria alipomuuliza sababu ya kumvunja moyo licha ya kusubiri kwa miaka minne.

Maria alijituliza kwa kuamini kwamba Mike hakuwa akimpenda kwa dhati na alichotaka kwake ni kumtumia tu.

“Kama kumuonjesha asali mwanamume kabla ya ndoa ndiyo leseni ya kuolewa, wacha nibaki mseja,” aliapa Maria.

Mwanadada huyo ni mmoja miongoni mwa wengi wanaokataliwa na wanaume kwa kukaa ngumu na kukataa kushiriki uroda kabla ya ndoa.

“Kuna wanawake walio na msimamo kwamba kamwe hawataruhusu mwanamume kuwaonja kabla ya ndoa. Wanaume wanaweza kusema hawapo lakini wapo,” asema Annita Nameme, mshauri wa wanandoa katika kituo cha Endurance Life jijini Nairobi.

“Inapaswa kuwa hivyo na sio uhalifu jinsi baadhi ya watu wanavyotaka wengine kuamini. Mwanamume anayekupenda kwa dhati atasubiri muoane kabla ya kukuonja. Ukiona mwanamume anataka kukusukuma kitandani mnapoanza uhusiano wenu, nafasi ya kukuoa huwa ndogo sana,” asema Nameme.

Hii ndiyo stori ya Jessica, mwanadada mwenye umri wa miaka 26 anayesema kwamba aliachwa na mchumba wake siku aliyokubali kumuonjesha tunda.

“Inaniuma sana. Hebu fikiria mwanamume uliyeishi naye kwa miaka mitatu mkipanga maisha ya siku za baadaye akikuacha baada ya kumpakulia asali. Unajiuliza maswali mengi sana,” akasema Jessica.

Kulingana na Nameme, wanawake wanafaa kung’amua kwamba mwanamume anayesubiri waoane ndipo walishane uroda ana heshima.

“Wengi huwa wanataka burudani tu. Wakichovya asali wanatoweka. Mwanamume anayependa kidosho kwa dhati huwa anaheshimu maamuzi yake. Akiamua kwamba hatakufungulia mzinga hadi mtakapofunga ndoa, heshimu uamuzi wake,” asema.

Bosco Otunga, mshauri wa vijana katika kanisa la Life Celebration Center, Nairobi, anasema kwamba wasichana wengi wamevurugiwa maisha na wanaume wanaowashawishi wawaonjeshe asali kabla ya ndoa.

“Visa vya wanawake kujuta baada ya kuachwa na wanaume baada ya kumeza chambo na kuwapa mili yao vimejaa kote. Wengi wao huachwa baada ya kupachikwa mimba na kubebeshwa mzigo wa ulezi. Ni heri kukaa ngumu kuliko kulegeza msimamo kuridhisha uchu wa mwanamume ambaye atakufanya ujute,” asema Otunga.

Anakubaliana na Nameme kwamba uroda sio leseni ya ndoa.

“Kama ungekuwa leseni ya ndoa, hakungekuwa na vilio vya wanawake kuachwa na wanaume wanaowapakulia asali,” asema.

Wataalamu wa masuala ya mapenzi wanasema kwamba watu wanaoana kabla ya kulishana asali huwa na ndoa yenye furaha.

Kulingana na utafiti uliochapishwa kwenye jarida la Journal of Family Psychology mwaka jana, maisha ya wanaochangamkia uroda kabla ya ndoa huishia kwa majuto.

“Watu wanaokosa kushiriki tendo la ndoa hadi usiku wanaofunga harusi huwa na ndoa zenye furaha na thabiti kuliko wale wanaolishana asali kabla ya ndoa,” inasema sehemu ya utafiti huo.

Otunga anasema kila lililoandikwa katika maandiko matakatifu huwa na sababu zake na huwafaidi wanaozingatia na kutimiza.

“Imeandikwa kuwa tendo la ndoa ni kwa mtu na mkewe na sio mtu na mkewe watarajiwa,” asema.

You can share this post!

Mshukiwa mkuu wa mauaji ya afisa wa NLC anyakwa

Zesco yazoa ushindi wa10 mfululizo ligini Zambia, Were,...