• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 6:27 PM
Changamoto tele wanafunzi wakirejea shuleni

Changamoto tele wanafunzi wakirejea shuleni

WANDERI KAMAU na FLORAH KOECH

WANAFUNZI wa shule za sekondari nchini wanarejea shuleni Jumatatu kwa muhula wa tatu, huku changamoto tele zikiendelea kuandama sekta ya elimu.

Licha ya serikali kutoa hakikisho kwamba kila kitu ki shwari, uchunguzi wa Taifa Leo umebaini kuwa, shule nyingi katika sehemu tofauti nchini bado hazijajitayarisha kukabiliana na maambukizi ya ugonjwa wa corona.

Kiwango cha maambukizi ya virusi hivyo nchini kingali zaidi ya asilimia tano. Katika baadhi ya maeneo, shule zina miundomsingi duni, uhaba wa walimu, ukosefu wa fedha kuziwesha kuendesha shughuli zake za kila siku na mafuriko makubwa.

Kwa mfano, katika Kaunti ya Baringo, hatima ya zaidi ya wanafunzi 4,000 haijulikani kutokana na ongezeko la visa vya ukosefu wa usalama.

Zaidi ya visa kumi vya mashambulizi vimeripotiwa katika eneo la Baringo Kusini kwa mwezi mmoja uliopita, ambapo watu wawili waliuawa.Miongoni mwa shule za msingi zilizoathirika ni Mukutani, Arabal, Kapindasum, Kasiela, Sinoni, Chebinyiny, Chemorong’ion, Noosukro, Sokotei na Kiserian katika eneo la Baringo Kusini.

Zingine ni Kagir, Yatya, Chemoe, Chepkesin, Barketiew, Kesumet, Kosile, Kapturo na Ng’aratuko katika eneo la Baringo Kaskazini.Hayo yanatokea wakati waziri wa Elimu, Prof George Magoha, anashikilia kuwa walimu wakuu hawapaswi kutoa visingizio vyovyote kuhusu changamoto zinazowaathiri, kwani serikali tayari ishatuma Sh7.5 bilioni kwa shule za msingi na upili za umma kuziwezesha kuendesha shughuli muhimu shuleni mwao bila matatizo yoyote.

“Tumeweka mikakati ya kutosha kuhakikisha wanafunzi wetu hawakabiliwi na matatizo yoyote wanaporejea shuleni,” akasema Profesa Magoha Ijumaa.

Licha ya waziri kusisitiza fedha hizo zimetumwa katika akaunti za shule, walimu wakuu waliozungumza nasi walisema bado hawajapokea fedha hizo na itawabidi kungoja ili kuona ikiwa zitatumwa kama alivyoahidi Waziri.

Serikali pia inakabiliwa na kibarua cha kuhakikisha walimu wote wamepewa chanjo dhidi ya virusi vya corona, ikizingatiwa kufikia sasa, ni nusu pekee ya walimu waliopewa chanjo hiyo.

You can share this post!

BBI: Kibarua kwa wabunge kushawishi wafuasi

Wapwani kukosa maji huku miradi ya Sh70b ikikwama