• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 2:16 PM
Wapwani kukosa maji huku miradi ya Sh70b ikikwama

Wapwani kukosa maji huku miradi ya Sh70b ikikwama

ANTHONY KITIMO, STANLEY NGOTHO na WACHIRA MWANGI

WAKAZI wa Mombasa, Kwale na Kilifi wataendelea kukabiliwa na uhaba wa maji baada ya miradi mitatu mikuu ya maji yenye thamani ya karibu Sh70 bilioni kukwama.

Licha ya kuwa na uungwaji mkono kutoka kwa Rais Uhuru Kenyatta, miradi hiyo ilikosa kuanza kwa wakati kwa kukosa ufadhili wa kutosha na mivutano kuhusu malipo ya fidia.

Mradi wa Mzima Spring II wenye thamani ya Sh35 bilioni, mradi wa Bwawa la Mwache wenye thamani ya Sh20 bilioni na kiwanda chenye thamani ya Sh16 bilioni, ilitarajiwa kusuluhisha matatizo ya maji yanayokabili kaunti hizo tatu.

Bwawa la Mwache lililopangiwa kuanza kujengwa mapema mwaka huu, limekumbwa na mizozo huku familia 2,452, taasisi nane za kijamii na umma zinazotazamiwa kufidiwa zikipanga kushtaki Tume ya Ardhi Nchini (NLC) kwa kutathmini mali yao isivyofaa na kuwalipa fidia duni.

Wakazi hao walishutumu NLC kwa kuwashawishi kukubali fidia ya Sh120,000 kwa kila ekari badala ya Sh350,000 jinsi ilivyoafikiwa hapo mbeleni.

“Hakuna maafikiano kati ya muuzaji na mnunuzi wa kujitakia kwa hiari na tunashinikizwa kufanya wanavyotaka, jambo ambalo ni la kusikitisha mno,” alisema mkazi kwa jina Uchi Mwero.

Gavana Salim Mvurya alisema wamekubaliana kuwasilisha kesi dhidi ya NLC kupitia njia mbalimbali wanazoweza ili kuhakikisha raia wanapata wanachostahili.

Alisema kuwa takriban wakazi 609 walioathiriwa miongoni mwa 624 katika eneo la ujenzi wa miradi hiyo linalozozaniwa la Fulugani, walishinikizwa kutia saini kiwango hicho duni cha fidia pasipo hiari yao.

Aidha, alieleza kwamba kundi lingine la wahasiriwa 736 katika eneo hilo walilazimishwa vilevile kutia saini malipo hayo duni.Kwingineko, wakazi katika vijiji kadhaa katika Kaunti Ndogo ya Kajiado ya Kati, wameachwa bila la kufanya baada ya maeneo hayo kukumbwa na mafuriko.

Mafuriko hayo yaliyotokea Jumamosi yalisomba daraja kadhaa na kuharibu barabara kiasi cha kutopitika.

Kutokana na mafuriko hayo, wakazi wa vijiji vya Torosei na Olongosua hawawezi kufika katika mji wa Illbisil kukunua vyakula na bidhaa nyingine muhimu kutokana na kiwango kikubwa cha maji kilicho kati ya maeneo hayo mawili.

Wanahofia huenda hali ikadorora zaidi, hasa baada ya barabara na daraja kuharibiwa.Wale waliokuwa mjini humo walilazimika kulala huko, huku watu waliokuwa wameenda katika soko la Torosei wakishindwa kurejea majumbani mwao.Wengine walikesha usiku kucha katika magari yao baada ya madaraja kusombwa.

Wanawake ndio walioathiriwa zaidi, hasa walio na watoto wachanga.“Tulilala kwenye magari chini ya baridi kubwa. Hatungeweza kurejea Torosei kutokana na hali mbaya ya barabara. Hatukula chalula chochote,” akasema Bi Jane Kores.

You can share this post!

Changamoto tele wanafunzi wakirejea shuleni

KONDOO WA RUTO MATAANI