• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 8:12 PM
Shule za Pwani zakosa kung’aa KCSE

Shule za Pwani zakosa kung’aa KCSE

Na WAANDISHI WETU

SHULE za Pwani zilikosa kung’aa katika matokeo ya Mtihani wa Kitaifa wa Shule za Upili yaliyotangazwa jana. Katika orodha ya watahiniwa 15 bora iliyotangazwa na Waziri wa Elimu, Prof George Magoha, hapakuwa na mwanafunzi yeyote kutoka kaunti za Pwani.

Vile vile, orodha ya watahiniwa 10 walioteleza katika matokeo ya Mtihani wa Kitaifa wa Shule za Msingi (KCPE) miaka minne iliyopita kisha wakabobea katika KCSE ya 2020, haikuwa na yeyote kutoka Pwani.

Kwa mujibu wa jedwali la matokeo ya shule za Pwani yaliyokusanywa na Taifa Leo, Assya Abubakar Ali ambaye ni msichana aliyesomea Shule ya Upili ya Sheikh Khalifa Bin Zayed, aliibuka nafasi ya kwanza akiwa na Gredi A ya alama 82.

Alifuatwa na Ashraf Mohammed Hassan wa Shule ya Upili ya Memon aliyepata Gredi A ya alama 81, na Sumayya Ahmed Mohammed wa Shule ya Upili ya Qubaa Muslim ambaye pia alipata alama sawa na hizo.Kitaifa, mwanafunzi aliyeibuka nafasi ya kwanza, Simiyu Robin Wanjala, mwanafunzi wa kiume aliyesoma katika Shule ya Upili ya Murang’a, alipata Gredi A ya alama 87.3.

Orodha ya 15 bora kitaifa ilifungwa na Buluma Daizy Nerima, mwanafunzi wa kike aliyepata Gredi A ya alama 86.9.Matokeo yaliyokusanywa na Taifa Leo, yalionyesha kuwa shule za kibinafsi za Pwani ndizo zilizotoa wanafunzi wengi waliopita mitihani hiyo.

Shule hizo ni Sheikh Khalifa Bin Zayed, Memon High, Qubaa Muslim, Abu Hureira na Istiqama High.Kwa upande mwingine, shule za umma zilizong’aa Pwani ni kama vile Dr Aggrey iliyo Kaunti ya Taita Taveta, Kwale High, Mambrui (Kaunti ya Kilifi), na Murray Girls (Taita Taveta).

Katika mahojiano na Taifa Leo, baadhi ya wanafunzi waliopata matokeo bora Pwani walieleza furaha yao huku wakiwa na matumaini kuhusu maisha yao ya usoni.

Nasia alisema kuwa alifanya bidii katika masomo yake na kuhoji kuwa ushirikiano mzuri baina ya walimu, wazazi na wanafunzi wenzake ulichangia kupata matokeo mazuri.

“Sikuwa natarajia kupata alama nzuri hivi kwani nilipata alama ya B kwenye mtihani wa majaribio. Lakini namshukuru Mungu kwa matokeo mazuri,’ alisema.

Alisema kuwa angependa kusomea udaktari katika Chuo Kikuu cha Nairobi.Ingawaje ugonjwa wa corona ulikatiza masomo shuleni kwa muda mrefu, msichana huyo alisema kuwa alifanya bidii hata akiwa nyumbani.

“Hii ilihakikisha kuwa nimesoma na kuwa tayari kufanya mtihani.Ninashukuru wazazi wangu kwa kufanya bidii kuhakikisha kuwa nilipata muda wa kutosha wa kusoma wakati wa likizo ndefu ya corona,” akasema.

You can share this post!

Wanafunzi 604, 031 kujiunga na mafunzo ya kiufundi

Walioteleza KCPE wawika katika KCSE