• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 9:40 PM
Wanafunzi wengi wakosa kuripoti shuleni baada ya daraja la Ngoliba kubomoka

Wanafunzi wengi wakosa kuripoti shuleni baada ya daraja la Ngoliba kubomoka

Na LAWRENCE ONGARO

DARAJA lililobomoka eneo la Ngoliba miezi mitatu iliyopita lilisababisha wanafunzi wengi kukosa kurejea shuleni mapema wiki hii.

Daraja hilo huunganisha kaunti za Kiambu na Murang’a.

Mwalimu mkuu wa Shule ya Upili ya Ngoliba iliyoko Thika Mashariki, Bi Esther Kamau alithibitisha kuwa wanafunzi wengi walikosa kufika shuleni huku wakihofia kuvuka hadi upande mwingine hapo kwa mashua kwa sababu mto Thika ulikuwa umevunja kingo zake.

“Wazazi wengi wamesema ni hatari kwa watoto kuvuka kwa sababu mto umefurika na kuna viboko hatari wanaopatikana hapo,” alisema Bi Kamau.

Alisema wanafunzi na wakazi wa maeneo hayo hulipa ada ya kati ya Sh50 na 20 kuvushwa kutoka upande mmoja hadi mwingine.

Chifu wa eneo hilo la Ngoliba Bi Alice Njoki amewashauri wakazi wa pande zote mbili wawe makini sana wanapopitia kwenye daraja hilo.

Alieleza ya kwamba wakazi wa maeneo hayo wanakadiria hasara kubwa kwa sababu kwa miezi hiyo michache biashara zao zimeyumba.

Alisema licha ya wakazi hao kutoa malalamiko yao kuhusu daraja hilo bado hakuna lolote la maana limefanyika.

“Kuna hatari kubwa ya wanafunzi kupitia daraja hilo kwa kutumia mashua kwa sababu mto Thika umefurika kwa sasa kutokana na mvua kubwa inayonyesha,” alisema chifu huyo.

Alieleza ya kwamba iwapo mvua kubwa inayonyesha itaendelea kwa wiki kadhaa, bila shaka biashara na masomo yatakwama kwa muda.

Alitoa wito kwa afisi ya ustawi wa eneobunge la Thika – NG-CDF – kufanya juhudi kuona ya kwamba daraja hilo linajengwa haraka iwezekanavyo.

Wahudumu wa bodaboda wamepata hasara kubwa kwa sababu hawawezi kusafiri hadi ng’ambo ya pili kubeba abiria. Bw George Mutisya anasema biashara ya uchukuzi imeyumba kwa sababu “hatuna kazi ya kufanya kwa wakati huu.”

“Tunataka viongozi wanaohusika na urekebishaji wa daraja hilo wafanye hima kuona ya kwamba kazi inaendeshwa mara moja ili shughuli zirejee kama kawaida,” alifafanua Bw Mutisya.

You can share this post!

Arsenal wazamisha chombo cha Chelsea uwanjani Stamford...

28,000 waliozoa ‘E’ KCSE bado wana fursa ya...