• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 6:55 PM
Wazazi watozwa ng’ombe 100 kwa utundu wa watoto wao

Wazazi watozwa ng’ombe 100 kwa utundu wa watoto wao

STEPHEN ODUOR na SIAGO CECE

WAZAZI wawili wametozwa faini ya ng’ombe 100 kwa jumla, baada ya watoto wao wenye umri wa miaka 15 na 17 kupatikana na hatia ya uasherati.

Wazee wa eneo la Kipini, Kaunti Ndogo ya Tana Delta walitoa uamuzi kuwa wazazi wa watoto hao walipe faini ya ng’ombe 50 kila mmoja.Kwa mujibu wa baraza la wazee, tabia ya watoto ilithibitisha wazazi hao, ambao tumewabana majina kwa sababu za kisheria, wameshindwa katika majukumu yao ya uzazi.

Walisema kitendo hicho ni haramu katika jamii na pia hakikustahili katika Mwezi Mtukufu wa Ramadhan.Zaidi ya hayo, wazazi waliagizwa kuwapeleka watoto hao kwa shule za bweni zilizopo mbali kwa miaka miwili ili kudhibiti tukio hilo kujirudia.

Endapo wazazi hao watashindwa kutii maagizo ya wazee, familia husika zitatengwa na kufukuzwa kutoka kwa jamii.“Tumeona madhara ya kutosha ya uasherati katika jamii yetu. Imechangia sana kwa ndoa za mapema, mimba za utotoni, na ndoa za utotoni na hata umaskini,” alisema Mzee Sadiq Salat.

Hata hivyo, wazazi waliopewa adhabu wamekata rufaa, wakisema ni zaidi ya uwezo wao kifedha.

“Ni tabia ambayo watoto wamekuwa wakifanya, jamaa wengine hata ?waliwaambia wazazi kuihusu ila wakafanya makusudi kuifumbia macho,” alisema mzee Ramadhan Ishmail.

Wazee walisema walituma vijana eneo hilo kufanya uchunguzi wa siri ndipo walipowafumania watoto hao wawili Jumatatu.Wazazi waliitwa kuelezea tabia ya watoto wao, huku wazee wakiongozwa na Ustadh Salim Maneno wakitanguliza kuwachapa viboko 20 kila mtoto kabla kuwapa ushauri nasaha.

Kwingineko, Serikali ya Kaunti ya Kwale imewahimiza vijana wajitenge na itikadi za kigaidi na utumizi wa mihadarati.Waziri wa masuala ya kijamii na ukuzaji wa talanta kaunti hiyo, Bw Ramadhan Bungale amewataka vijana kujiunga na vyuo vya kiufundi ili kupata ujuzi wa kujiendeleza kimaisha.

Kaunti hiyo ni moja ya zile zilizo na idadi kubwa ya vijana wanaotumia mihadarati inayofanya wengi kujihusisha na uhalifu.“Vijana wengi wanajihusisha na mihadarati kwa sababu ya kukosa kazi, wakipata ujuzi huu wataweza kujitegemea na hawatakua na tamaa ya kutumia dawa hizo,” alieleza Bw Bungale.

You can share this post!

Ruto alenga waasi wa Odinga Luo Nyanza

Watoto zaidi ya 2,000 waambukizwa HIV kwa kunyonyeshwa