• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 4:28 PM
Kufanikisha refarenda sasa ni kama kushuka mchongoma

Kufanikisha refarenda sasa ni kama kushuka mchongoma

Na BENSON MATHEKA

Rais Uhuru Kenyatta ana nafasi finyu ya kisheria kutimiza ndoto ya kubadilisha katiba baada ya Mahakama Kuu kuamua alikiuka katiba katika maamuzi yake.

Ingawa anaweza kukata rufaa, itakuwa vigumu kwa kesi kuamuliwa kabla ya muda uliopangwa refarenda ifanyike. Waandalizi wa BBI walipanga kura ya maamuzi ifanyike kabla ya Agosti mwaka huu na utekelezaji wa baadhi ya mabadiliko yaliyopendekezwa ufanyike kabla ya uchaguzi mkuu ujao.

Wataalamu wa katiba na wanaharakati wanasema nafasi ya kukomboa mchakato huo ni finyu sana kwa kuwa walalamishi wanaweza kuwasilisha ombi katika Mahakama ya Juu iwapo korti ya rufaa itasimamisha uamuzi wa majaji wa Mahakama Kuu.

“Kwa maoni yangu haya ya BBI yamekwisha na Rais Kenyatta anafaa kusalimu amri tu na kusubiri amalize kipindi chake uongozini kwa amani,” asema Elias Mutuma. Wakili huyu anasema ikizingatiwa uamuzi huo ulitolewa na majaji watano, huenda ikawa vigumu kwa Mahakama ya Rufaa kuubatilisha.

Ingawa Rais Kenyatta amekuwa akipuuza maamuzi na maagizo ya korti, wanasheria wanasema kukaidi uamuzi kuhusu BBI kunaweza kumuacha na aibu zaidi.

Wanasema akitumia njia ya mkato na mchakato uendelee, kuna hatari ya Wakenya kuukataa katika refarenda kwa sababu mahakama imewafungua macho wakafahamu una nia fiche. “Uamuzi ulikuwa wa kina na nafasi anayoweza kupata ni kusimamishwa kwa uamuzi huo kupitia rufaa.

Hata hivyo, mfumo wa sheria na muda hauko upande wake na hatua atakayochukua itakuwa ya mabavu jambo ambalo litaendeleza sifa zake za kukaidi mahakama na utawala wa sheria,” asema mwanaharakati Oscar Ojiambo.

Baadhi ya maamuzi ambayo rais amepuuza ni kuapisha majaji 41 ambao waliteuliwa na Tume ya Huduma ya Mahakama yapata miaka miwili iliyopita, kumruhusu wakili Miguna Miguna kurudi Kenya, kuvunja bunge kwa kutotimiza hitaji la usawa wa jinsia.

Mahakama pia iliamua kwamba Idara ya Huduma ya Jiji la Nairobi lilibuniwa kinyume cha sheria. Mwezi jana, mahakama iliamua kwamba nyadhifa za mawaziri wasaidizi alizobuni sio za kikatiba lakini akapuuza.

Kulingana na Gavana wa Makueni Kivutha Kibwana uamuzi wa majaji Joel Ngugi, George Odunga, Jairus Ngaah, Teresiah Matheka na Chacha Mwita ni wa kizalendo na ni vigumu kukata rufaa kuupinga. Majaji hao walikosoa kila kitu kuhusu BBI na kuendelea na mchakato huo itakuwa ni kilele cha ukaidi.

You can share this post!

Uamuzi wa mahakama wavuruga urithi wa Uhuru 2022

Karua na kundi la Tangatanga walivyoungana kushambulia BBI