• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 9:55 AM
JAMVI: Mbio za Ngilu kutuliza zogo, uasi katika ODM

JAMVI: Mbio za Ngilu kutuliza zogo, uasi katika ODM

HATUA ya Gavana Charity Ngilu wa Kitui ya kukutanisha Kiongozi wa chama cha ODM Raila Odinga na washirika wake James Orengo, Otiende Amollo na Wycliffe Oparanya walipotofautiana kuhusu mswada wa BBI kabla ya kuharamishwa na mahakama zilituliza joto katika uongozi wa chama hicho cha chungwa.

Baada ya kuona hatari iliyokodolea macho washirika wake wa kisiasa wa miaka mingi, Bi Ngilu aliwasiliana na pande zote na wakapanga kukutana kwa Bw Odinga ambapo alihimiza umuhimu wa kudumisha umoja katika chama hicho kikubwa cha upinzani.

Kabla ya mkutano huo, Bw Orengo na Bw Otiende walikuwa wametofautiana na msimamo wa viongozi wa ODM bungeni kuhusu pendekezo la kubuniwa kwa maeneo bunge mapya 70.

Msimamo wao ulichukuliwa kama uasi ikizingatiwa kwamba Bw Odinga alikuwa akiunga pendekezo hilo na kuagiza wabunge wote wa ODM kuunga mswada huo.

Hali ilizidi kuwa mbaya pale Bw Otiende aliposusia mkutano ambao Bw Odinga aliitisha nyumbani kwake na ikabidi apokonywe wadhifa wake wa Naibu mwenyekiti wa Kamati ya bunge kuhusu sheria (JLAC).

Hii ilikuwa siku moja baada ya kukutana na Bw Oparanya nyumbani kwake Kakamega. Ikizingatiwa kuwa baadhi ya wandani wa Bw Odinga walishuku uhusiano wa Gavana huyo na Naibu Rais William Ruto, mkutano wa watatu hao ulizua taharuki ndani ya ODM kwamba walikuwa na njama dhidi ya ODM na Bw Odinga.

Duru zinasema kuwa Bi Ngilu aliwaambia wanasiasa hao kwamba walikuwa wakitoa picha mbaya kwa kuanika wazi tofauti za chama chao hasa baada ya kumvua Bw Otiende wadhifa wake katika JLAC. Kulingana na wandani wa gavana huyo, ni viongozi hao watatu wa ODM waliomuomba Bi Ngilu kuzungumza na Bw Odinga.

“Mama ameshirikiana kisiasa na wanasiasa hao na kwa vile hawangeweza kumkabili baba kufuatia madai kwamba walikuwa wameasi msimamo.wake walimuomba awe mpatanishi,” alisema msaidizi wa Bi Ngilu ambaye aliomba tusitaje jina lake.

Bi Ngilu hakukanusha wala kukubali kuwa alikutanisha viongozi hao kwa Bw Odinga.?“Tulizungumzia masuala kadhaa kutoka BBI, siasa na hali ya sasa ya janga la corona nchini. Tulikubaliana kwamba kuna haja ya dharura ya kuendelea kuungana kwa kuwa kuna adui mkubwa mbele yetu,” Bi Ngilu alisema baada ya mkutano huo.

Gavana huyo ambaye ni kiongozi wa chama cha Narc alisema kwamba muhimu kwake ni kuona nchi ikiwa imeungana.?“Sisi sote tunataka kilicho bora kwa Wakenya,” alisema bila kufafanua zaidi.

Duru zinasema kwamba japo joto ilipanda kwenye mkutano huo, Bi Ngilu aliweza kuwapatanisha na Bw Odinga.?Viongozi hao walimhakikishia Bw Odinga kwamba wangali waaminifu kwa chama cha ODM na sio waasi inavyochukuliwa walipokosoa BBI.

Mnamo Alhamisi, mahakama kuu ilitaja kubuniwa kwa maeneobunge 70 ambayo viongozi hao walikosoa katika BBI kuwa haramu. Pia ilisema mchakato wote wa BBI ulikuwa haramu.

Inasemekana kwamba Bw Orengo na Bw Otiende walishikilia kuwa kauli zao kuhusu mchakato huo zilitokana na tajiriba yao ya uanasheria na sio kudharau viongozi wa vyama.

Japo inasemekana Bi Ngilu aliwaacha wakijadili masuala ya ndani ya ODM uhusiano wake na viongozi hao na msimamo wake wa kisiasa umefanya wamuamini. Yeye na Bi Ngilu wamewahi kuwa wanachama wa chama cha Social Democratic Party SDP miaka ya tisini. Bw Orengo, Oparanya na Bi Ngilu walihudumu katika baraza la mawaziri katika serikali ya muungano wa Narc mwaka wa 2003 kwa hisani ya Bw Odinga?.

“Wako na historia ndefu ya uhusiano wa kisiasa na kumtumia Bi Ngilu kuwapatanisha au kuwaombea radhi kwa Bw Odinga ni kutambua uwezo wake. Kwa kuwa anatoka nje ya ngome zao za Nyanza na Magharibi na ikizingatiwa msimamo wake wa kisiasa kulisaidia kurekebisha hali katika chama hicho cha upinzani,” alisema mchanganuzi wa siasa David Wanyama.

Baada ya mkutano huo, ODM kilisema kimemrejesha Otiende katika JLAC ingawa nafasi yake ilikuwa imetwaliwa na mbunge wa Ruaraka TJ Kajwang. Bw Oparanya alikiri kwamba mkutano huo ulikuwa wa kuzima hofu kwamba wameasi ODM.

“Mkutano wetu unafaa kuondoa uvumi kwamba kuna uasi katika ODM kwa kuwa haya ni madai ya mahasimu wetu wa kisiasa. Nashukuru dada yetu Mheshimiwa Ngilu kwa usaidizi wake,” alisema.

You can share this post!

Zidane kuagana na Real Madrid mwishoni mwa msimu

JAMVI: Mwaura alivyojikwaa na kujiponza kisiasa