• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:33 AM
Uhuru apangiwa kuzuru Pwani baada ya Raila

Uhuru apangiwa kuzuru Pwani baada ya Raila

ANTHONY KITIMO na CHARLES LWANGA

RAIS Uhuru Kenyatta anatarajiwa kuzuru Pwani wiki hii, siku chache baada ya Mahakama Kuu kuharamisha urekebishaji katiba kupitia Mpango wa Maridhiano (BBI).

Ingawa ratiba rasmi kuhusu ziara ya rais haijatolewa, anatarajiwa kutembelea miradi ya maendeleo katika ukanda huo.

Kufikia jana, Rais Kenyatta alikuwa hajaeleza hisia zake kuhusu uamuzi wa majaji watano wa Mahakama Kuu kuharamisha BBI.

Kwa upande mwingine, ilifichuka kuwa mwasisi mwenzake wa BBI aliye kiongozi wa Chama cha ODM, Bw Raila Odinga tayari alikuwa ametua Pwani wikendi.

Hata hivyo, duru ziliambia Taifa Leo kwamba ziara ya Bw Odinga Kaunti ya Kilifi ilikuwa ya kibinafsi na bado haijulikani kama watakutana na rais atakapowasili.

Mnamo Jumamosi, alikutana na naibu mwenyekiti wa chama cha Jubilee David Murathe, Katibu Mkuu Muungano wa vyama vya wafanyakazi Francis Atwoli, Magavana Ali Joho (Mombasa) na Amason Kingi (Kilifi) miongoni mwa wanasiasa wengine. Mkutano huo ulitajwa kuwa wa chakula cha mchana.

Matarajio makuu kuhusu ziara yake ya Pwani ni kwamba atasimamia kushuhudiwa kwa meli mbili za kwanza za usafirishaji mizigo zikitia nanga katika Bandari ya Lamu mnamo Alhamisi.

Meli ya Mv CAP Carmel yenye urefu wa mita 204 inayotarajiwa kusafirisha mizigo mbalimbali kutoka Dae es Salaam, itakuwa ya kwanza kutia nanga Lamu kabla ielekee Bandari ya Salalah iliyo Oman baadaye.

Meli ya pili iliyopangiwa kutia nanga hapo dakika chache baadaye ni ile ya Mv Seago Bremen Kaven kutoka Mombasa ambayo itakuwa ikisafirisha parachichi.

Mamlaka ya Kusimamia Bandari za Kenya (KPA) pamoja na Mamlaka ya Ukusanyaji Ushuru (KRA) tayari zimeanza kutamatisha mipango muhimu kabla hafla hiyo inayotarajiwa kubadilisha uchumi wa Pwani na Kenya kwa jumla.

Kapteni Geoffrey Namadoa kutoka KPA alisema MV CAP Carmel ambayo ina bendera ya Singapore, ina uwezo wa kupakia na kupakua mizigo bandarini bila kutumia kreni.

“Kulingana na orodha ya shehena tuliyopokea, tunatarajia kuhudumia kontena 100 za meli katika siku ya kwanza bandarini Lamu. Shehena hizo zitatumiwa kufanyia majaribio barabara inayoelekea bandarini ambayo ujenzi wake umekamilika,” akasema Bw Namadoa.

Alieleza kuwa bandari hiyo imejengwa mahali pazuri ambapo itakuwa mshindani mkubwa wa bandari nyingine zilizoendelea kimataifa kama vile ya Durban, Afrika Kusini.

Kwa upande mwingine, meneja mkuu wa kitengo cha huduma za baharini katika KRA, Bw John Bisonga, alisema wanakamilisha kuweka mitambo ambayo itazuia usafirishaji wa bidhaa haramu kupitia kwa Bandari ya Lamu.

“KRA inafahamu fika kwamba wahalifu huenda wakajaribu kutumia bandari ya Lamu kwa shughuli zisizokubaliwa kisheria lakini tumepeleka rasilimali zote zinazohitajika ikiwemo wahudumu na mitambo,” akasema.

Kando na kutumia mitambo ya kitekinolojia, Bw Bisonga alisema kutakuwa pia na mbwa wa kunusanusa iwapo hilo litahitajika mara kwa mara.

Serikali imewapa wafanyabiashara vichocheo vya kuwavutia ikiwemo uhifadhi mizigo kwa siku 60 bila malipo kwa wanaosafirisha bidhaa kupitia Lamu, badala ya siku 21 ambazo hutolewa katika Bandari ya Mombasa.

You can share this post!

Wetang’ula awatetea majaji 5 kuhusu BBI

Serikali yaonya dhidi ya fujo katika uchaguzi wa Bonchari