• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 9:40 PM
UDAKU: Dele Alli si mchache! Ameingiza boksi binti wa kocha Guardiola

UDAKU: Dele Alli si mchache! Ameingiza boksi binti wa kocha Guardiola

Na CHRIS ADUNGO

MIEZI miwili baada ya Dele Alli kutemwa na kipusa Ruby Mae, kiungo huyo wa Tottenham Hotspur na timu ya taifa ya Uingereza amepata hifadhi kwa Maria, ambaye ni binti ya kocha wa Manchester City, Pep Guardiola.

Alli, 25, alionekana na Maria wiki jana wakiponda raha ya ujana katika hoteli ya kifahari ya Cloud 9 jijini London, Uingereza.

Wawili hao walishiriki vileo kabla kuanza kukumbatiana, kupapasana na kupokezana mabusu motomoto mbele ya mamia ya wateja katika mkahawa huo maarufu.

Hadi walipoondoka hotelini, Maria, 20, alioonekana kujilegeza kimapenzi huku mkono wa Alli ukisisimuana na kiuno chake cha nyigu. Naye Maria akatuliza mkono kwenye bega la Alli – tukio lililoleta taswira ya mapenzi kati ya wapenzi wawili waliostahiana.

Akihojiwa na gazeti la The Sun, msemaji wa familia ya Alli alifichua kwamba mwanasoka huyo alianza kumtambalia Maria kimapenzi mwanzoni mwa Aprili; mwezi mmoja baada ya kuzidiwa na kijibaridi cha ukapera kufuatia kuondoka kwa Ruby.

“Penzi lao linazidi kunoga na Maria amekuwa akimtembelea Alli mara kwa mara. Alli na Maria bado ni wachanga. Kila mmoja yuko huru na huenda huu ni mwanzo wa safari ya ndoa baina yao,” msemaji huyo alinukuliwa.

Maria ni mwanafunzi jijini London ila pia ana maazimio ya kujitosa katika ulingo wa uanamitindo.

Ndiye kifungua mimba katika familia ya watoto watatu wa Guardiola na mkewe Cristina Serra, aliye mfanyabiashara maarufu nchini Uhispania.

Kwa mujibu wa gazeti la Mirror Sport nchini Uingereza, Alli alikutana na Maria kupitia App ya kusaka wapenzi ya Raya, kila mmoja akiwa anatafuta mpenzi.

Alli alijiunga na App hiyo wiki kadhaa baada ya kutemwa na Ruby – mwanamitindo aliyedai kwamba kiungo huyo alitumia muda wake mwingi kushiriki michezo mitandaoni na kumwachia baridi ya upweke usiku kucha.

Guardiola na Cristina walichumbiana kwa miaka 20 kabla ya kufunga pingu za maisha mnamo 2014 baada ya kuzaliwa kwa watoto wao – Maria, Marius, 18, na Valentina, 13.

Kwa mujibu wa gazeti la Mirror Sport nchini Uingereza, Alli alikutana na Maria kupitia programu ya mitandaoni, Raya, kila mmoja akiwa anatafuta mpenzi.

Alli alijiunga na ‘App’ hiyo inayohusishwa na mabwanyenye wiki kadhaa baada ya kutemwa na Ruby – mwanamitindo aliyedai kwamba kiungo huyo alikuwa akitumia muda wake mwingi kushiriki michezo ya mitandaoni na kumwachia baridi ya upweke usiku kucha.

“Nilichoshwa na mienendo ya Alli ambaye alikuwa amemezwa na michezo ya video na vibonzo aina ya Fortnite,” akasema Ruby.

Ruby ambaye amewahi kuwa balozi wa mauzo wa bidhaa za Dolce & Gabbana pamoja na Chanel, alianza kutoka kimapenzi na Alli mnamo 2016 na wakatengana kwa mara ya kwanza mnamo 2018 kabla ya kurudiana.

Kiini cha kutengana kwao kwa mara ya kwanza ni jicho kali la nje la Alli aliyeanza kuchovya asali kwenye mzinga wa mwigizaji maarufu Megan Barton-Hanson anayemzidi umri kwa mwaka mmoja. Alli alianza kuburudishwa na Megan mwezi mmoja baada ya kichuna huyo mwenye umri wa miaka 26 kutemana na mwigizaji mwenzake wa filamu za Love Island, Wes Nelson, 23.

You can share this post!

AC Milan watoka sare dhidi ya Cagliari kwenye Serie A

Celta Vigo yazamisha matumaini finyu ya Barcelona kutawazwa...