• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Chebukati ashuhudia maandalizi ya uchaguzi wa Juja

Chebukati ashuhudia maandalizi ya uchaguzi wa Juja

Na LAWRENCE ONGARO

TUME Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), ilikamilisha maandalizi yake Jumatatu ambapo katika shule ya upili ya Mang’u High, maafisa wake walihakikisha vifaa vya uchaguzi wa eneobunge la Juja vilikuwa tayari.

Maafisa wa uchaguzi wa IEBC walionekana wakiendelea na mikakati ya kupanga masanduku ya kura na kuyasambaza katika vituo 184.

Mwenyekiti wa IEBC Wafula Chebukati, alifika katika kituo kikuu cha shule ya upili ya Mang’u High na kusema mipango yote iko shwari.

Alisema chaguzi mbili za ubunge za Juja na Bonchari, Kisii zitaendelea kama kawaida licha ya kizingiti kilichowekwa na mahakama kuu kuwa tume hiyo haistahili kuendesha uchaguzi wowote kutokana na idadi chache ya makamishna walioko afisini. Kwa sasa ina makamishna watatu.

“Uamuzi uliotolewa na mahakama hapo awali, wa mwaka wa 2019, ni kwamba mahakama kuu ilisema ya kwamba afisi ya IEBC inaweza kuendesha uchaguzi na maafisa watatu afisini na kwa hivyo tutaendelea na chaguzi hizo mbili,” alisema Chebukati.

Hata hivyo alisema tume hiyo itapinga uamuzi uliotolewa Alhamisi wiki jana na mahakama kuu ambapo majaji watano walitoa hukumu kuhusu uhalali wa afisi yao yenye makamishna watatu walioko kwa sasa baada ya wengine kujiuzulu.

Alisema maafisa wa usalama wamewekwa wa kutosha ambapo ana imani ya kwamba kila kitu kitaendeshwa jinsi ilivyopangwa.

Alisema uchaguzi huo wa Juja ungeng’oa nanga saa kumi na mbili za alfajiri hadi saa kumi na moja jioni ambapo baadaye wataanza kuhesabu kura katika ukumbi mkuu wa shule ya Mang’ u High.

Uchaguzi huo umevutia wawaniaji 10 huku ushindani mkali ukitarajiwa kuwa kati ya Bi Susan Njeri Waititu, mkewe marehemu Francis ‘Wakapee’ Waititu, wa chama cha Jubilee na Bw George Koimburi wa chama cha People Empowerment Party (PEP) kinachohusishwa na mbunge wa Gatundu Kusini Moses Kuria.

Kulingana na sheria na kanuni za afya mikutano ya watu wengi ilipigwa marufuku kama njia mojawapo ya kupunguza kuenea kwa Covid-19.

Hali hii ilisababisha wawaniaji wengi kuwa na changamoto ya kukutana na umati mkubwa wa wananchi kuwashawishi.

Afisa mkuu wa IEBC wa Juja Bw Justus Mbithi, amewahimiza wapigakura zaidi ya 115,000 kujitokeza kwa wingi ili kumchagua kiongozi wanayemtaka.

You can share this post!

Maandamano yaandaliwa Mombasa kulaani Israeli kwa mauaji ya...

Wakazi wa Nyandarua waadhimisha Siku ya Punda Nchini