• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
FAUSTINE NGILA: Serikali isikimye gharama ya intaneti ikizidi kupanda

FAUSTINE NGILA: Serikali isikimye gharama ya intaneti ikizidi kupanda

NA FAUSTINE NGILA

IWEJE Kenya, taifa linalotambuka Afrika kwa mpenyo wa juu wa intaneti, inaburuta mkia katika orodha ya mwaka huu ya gharama ya vifurushi vya data Afrika Mashariki?

Binafsi ninaishangaa serikali kukubalia kampuni za mawasiliano kuwapunja Wakenya katika kipindi ambapo uchumi wa nchi umezorota kutokana na athari za janga la Covid-19.

Kama hauna habari, basi ng’amua kwamba kwa wastani, unalipa Sh244 kwa kila 1GB ya intaneti ya simu kulingana na takwimu zilizotolewa majuzi na kampuni ya utafiti ya Cable ya Uingereza.

Hii ni maradufu ya Sh112 ambazo wananchi walikuwa wanalipa mwaka uliopita, na hii sasa imefanya Kenya kuwa nyuma ya Tanzania, Rwanda, Uganda na Burundi hapa Afrika Mashariki.

Watanzania wanalipa Sh81 tu na hata taifa linaloongoza barani Afrika, Sudan, linalipisha Sh29. Yamaanisha inawezekana kupunguza bei ya data bila kuathiri sekta zingine, ila serikali imeziachia Safaricom, Airtel na Telkom fursa ya kuongeza bei badala ya kupunguza.

Najua wajiuliza imekuwaje kuwa data hii ni ghali ilhali unalipa Sh1,000 kupata 60GB za Telkom au 75GB za Airtel.

Ukweli ni kwamba kampuni hizi zinatumia teknolojia za kisasa kuchanganua watumizi wa intaneti ya simu. Zimetambua kuwa wananchi wanaotumia chini ya Sh50 kununua intaneti ndio wengi na hivyo kuifanya kuwa ghali na kuisha haraka.

Kwa Sh20, utapata 70MBs tu kwenye Safaricom na zitaisha haraka usivyotarajia, kumaanisha umeuWakenziwa data ya 40Mbs ila arafa inaonyesha 70Mbs.

Kwa wanaolipa Sh1,000 kwenda juu, wanapewa intaneti ya kasi na unayoweza kutegemea, ila ni watu wachache tu wanaweza kumudu bei hiyo. Wanalenga walio chini ndipo waunde mamilioni kwa kuhakikisha data inaisha haraka.

Sababu nyingine ni kuwa Safaricom ndiyo inaongoza kwa mtandao wa mawimbi nchini, hivyo watu wengi hutumia data ya kampuni hiyo ambayo ni ghali. Telkom na Airtel, kwa upande wao, bado wanakabiliwa na upungufu wa mawimbi katika sehemu za mashinani. Ikiwa ulikuwa umenunua intaneti yao na ukasafiri Samburu, basi itabidi ugeukie Safaricom ununue intaneti tena.

Ni mtindo huu ambao umepandisha bei ya data bila kujali kuwa Wakenya wana majukumu mengine ambayo tayari ni ghali. Wengi wamepoteza ajira kutokana na janga la corona na kupata hela za lishe, kodi ya nyumba, matibabu au karo imekuwa changamoto kuu.

Ni wakati wa serikali kugundua kuwa ingawa Wakenya wamefinywa na hali ngumu ya maisha, bado wanahitaji kupata taarifa zinazowahusu kwenye mitandao na bei ya huduma hiyo inafaa kupunguzwa.

Sudan au Somalia ni mataifa yenye uwezo mdogo wa kiuchumi kuliko Kenya, lakini wananchi wake wanafurahia intaneti kwa bei nafuu zaidi. Hii inaaamisha gharama ya kufanya utafiti au kuwekeza kwa huduma za mitandaoni iko chini. Ni nini mataifa hayo yamefanya ambacho Kenya haiwezi kutekeleza?

Hapa Kenya, inaonekana bei ya kila kitu imepanda tangu janga hili lianza kututafuna. Bei ya mkate, unga, mafuta, huduma na sasa intaneti imepanda bila serikali kufanya chochote.

Iwapo serikali itaendelea kuziacha kampuni hizi kunyanyasa Wakenya, basi hata mwaka ujao tutalipa zaidi ya Sh300 kwa kila 1GB ya data. Ni jukumu la serikali kutumia ushuru inaokata wananchi kuwalinda dhidi ya dhuluma hizi.

You can share this post!

COVID-19: Aina inayoangamiza India yagunduliwa Kenya

Nilipoteza kilo nne nilipougua malaria baada ya kuchezea...