• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 10:55 AM
Rais Biden sasa ataka Israeli isitishe mashambulio Gaza

Rais Biden sasa ataka Israeli isitishe mashambulio Gaza

Na MASHIRIKA

GAZA, Palestina

RAIS wa Amerika Joe Biden, Jumanne alieleza hisia zake kuhusu kusitishwa kwa mapigano baada ya siku nane za ghasia za kikatili kati ya jeshi la Israeli na wanamgambo wa Palestina mjini Gaza.

Biden aliambia Waziri Mkuu wa Israeli Benjamin Netanyahu kwamba Amerika inashirikiana na Misri na mataifa mengine kusitisha machafuko hiyo.

Hata hivyo, Amerika kwa mara nyingine ilizuia taarifa ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, iliyoitisha kusitishwa kwa mapigano hayo.

Rais wa Amerika Joe Biden. Picha/ AFP

Ghasia hizo sasa zimeingia katika wiki yake ya pili bila dalili zozote za kusitishwa.

Israeli mapema Jumanne iliendeleza mashambulio yake ya angani dhidi ya Gaza.

Jeshi lake lilisema mamia ya roketi zilifyatuliwa katika eneo lake usiku kucha. Watu wasiopungua 212 wakiwemo wanawake na watoto 100 wameuawa Gaza, kulingana na wizara ya afya nchini humo.

Katika taifa la Israeli, watu 10 ikiwemo watoto wawili wameuawa kulingana na idara ya matibabu humo.

Israeli ilisema Jumanne kuwa wanamgambo wapatao 150 ni miongoni mwa waliouawa Gaza.

Kundi la Hamas, ambalo ni wanamgambo wa Palestina wanaotawala eneo hilo, huwa halitoi idadi ya wapiganaji waliojeruhiwa.

Kulingana na taarifa kutoka Ikulu ya White House mnamo Jumatatu, Biden “alihimiza Israeli kujitahidi kwa vyovyote vile kuhakikisha ulinzi wa raia wasio na hatia.”

“Viongozi hao wawili walijadili kuhusu maendeleo katika oparesheni za jeshi la Israeli dhidi ya Hamas na makundi mengine ya magaidi mjini Gaza. Biden alieleza kuunga mkono kusitishwa kwa mapigano na akajadili ushirikiano wa Amerika, Misri na mataifa mengine kuhusu suala hilo,” ilisema taarifa.

Viongozi wa dunia na mashirika ya kutoa msaada wa kibinadamu wameitisha mikakati ya kuzuia vifo vya wakazi na ghasia zinazosababishwa na uharibifu wa majengo na miundomsingi.

Amerika, ambayo ni mojawapo wa marafiki wakuu zaidi wa Israeli, kwa mara nyingine ilizuia juhudi za Baraza la Usalama la Umoja wa Mataiga kutoa taarifa ya kuitaka Israeli kusitisha mashambulizi yake, na badala yake ikasisitiza juhudi zake za kidiplomasia.

“Makisio yetu kwa wakati huu ni kwamba, kuwa na mazungumzo hayo faraghani…ndio mwelekeo mwafaka zaidi tunaoweza kuchukua,” Msemaji wa White House Jen Psaki alieleza wanahabari.

Baraza la Usalama la UN linatazamiwa kushiriki mkutano wake wa dharura kuhusu ghasia hizo Jumanne.

UN pia ilielezea wasiwasi wake kuhusu uharibifu wa miundomsingi katika eneo linaloandamwa tayari na ufukara la Ukanda wa Gaza.

You can share this post!

Utalii: Balala apingwa kuhusu ubinafsishaji

Benzema sasa kuchezea Ufaransa kwa mara ya kwanza tangu 2015