• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 3:03 PM
Vigogo wa Pwani lawamani kwa maneno matupu

Vigogo wa Pwani lawamani kwa maneno matupu

Na CHARLES LWANGA

VIONGOZI wakuu Pwani wako hatarini kupata sifa mbaya ya kukosa kuonyesha vitendo kwa mipango ya kisiasa ambayo huwa wanahimiza kwa wananchi mara kwa mara.

Miaka mitatu iliyopita, Gavana wa Kilifi Amason Kingi na mwenzake wa Mombasa Hassan Joho, walifufua wito wa kuitaka Pwani ijitenge na Kenya walipokuwa wakipinga utawala wa Rais Uhuru Kenyatta.

Hata hivyo, wito huo ulififia baada ya Rais Kenyatta na Kiongozi wa ODM Raila Odinga kukubaliana kushirikiana kupitia mpango wao wa handisheki baadaye 2018.

Bw Joho husisitiza kuwa hapakuwa na haja kuendeleza mtindo huo wa kisiasa kwani walipewa nafasi ya kushauriana moja kwa moja na serikali kuu kuhusu changamoto zinazokumba Wapwani.

Hali sawa na hii sasa inaelekea kukumba wito wa uundaji chama au muungano mmoja wa vyama vya Pwani kabla Uchaguzi Mkuu wa 2022.

Wito huo uliokuwa umeanza kwa kishindo umezidi kufifia baada ya Bw Joho kujiandikisha kupigania tikiti ya ODM kuwania urais 2022.

Kwa upande mwingine, wanasiasa wengine wameashiria kujiunga na Chama cha United Democratic Alliance (UDA) ambacho kinahusishwa na Naibu Rais William Ruto.

Wanasiasa hao wakiongozwa na Mbunge wa Malindi, Bi Aisha Jumwa, tayari wameunda kamati maalumu itakayopendekeza kiongozi wa Pwani ambaye jina lake litawasilishwa kwa Dkt Ruto kumzingatia kama mgombea mwenza wake, na pia itatoa ripoti kuhusu matarajio ya Wapwani kutoka wa naibu rais iwapo ataunda serikali ijayo.

Kando na hayo, juhudi za viongozi wa kaunti sita za Pwani kushirikiana katika sera hasa za kuimarisha uchumi kupitia kwa Jumuiya ya Kaunti za Pwani (JKP) pia zimeonekana kwenda mwendo wa kobe.

Mnamo Februari, wakati Gavana wa Taita Taveta Granton Samboja alipochaguliwa kuwa mwenyekiti wa JKP, iliwabidi magavana kutoa wito kwa wadau husika wakaze kamba zaidi kufanikisha maazimio ya jumuiya hiyo.

Kulingana na Bw Steve Obaga, ambaye ni mchanganuzi wa kisiasa Malindi, kuna uwezekano wanasiasa Pwani bado hawana hakika kama wana uwezo wa kutosha kushindana na vyama vingine vikubwa kama vile ODM, Wiper na Jubilee ndiposa juhudi zao za kuungana hugonga mwamba.

Bw Obaga anasema kuwa, kuungana kwa wanasiasa hao kutamaanisha watahitajika kushindana na vyama hivyo ambavyo havitakosa wagombeaji uchaguzini.

“Wapwani wana desturi ya kuwa hawaungi mkono vyama vya eneo hilo. Hata marehemu Karisa Maitha aliyekuwa mbunge wa Kisauni, alijaribu kuleta umoja ukanda huo lakini hakufanikiwa,” akasema.

Kando na Maitha, juhudi kama hizi ziliwahi kujaribiwa miaka mingi iliyopita zikiongozwa na aliyekuwa kiongozi wa Chama cha Kenya African Democratic Union (Kadu), Ronald Ngala.

You can share this post!

Mbunge mpya wa Juja ni Koimburi wa PEP

Watabiri hewa Pwani wachanganya wakazi