• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 1:29 PM
Uhuru na Raila kusafiri kwa garimoshi hadi jijini Kisumu

Uhuru na Raila kusafiri kwa garimoshi hadi jijini Kisumu

Na RUSHDIE OUDIA

RAIS Uhuru Kenyatta na kiongozi wa chama cha ODM, Raila Odinga, wiki ijayo wanatarajiwa kufanya safari ya kwanza ya gari la moshi kutoka Naivasha hadi Kisumu kufungua reli ya zamani iliyokarabatiwa.

Kulingana na duru, baada ya kufika Kisumu, kiongozi wa nchi na Bw Odinga wanatarajiwa kufungua kituo kipya cha reli karibu na kiwanda cha nguo cha Kisumu Cotton Mills (Kicomi).

Huu ni mmoja wa miradi ambayo Rais Kenyatta atafungua katika ziara yake ya siku tano katika jiji la Kisumu.

Pia atafungua bandari ya Kisumu, uwanja wa michezo wa Jomo Kenyatta uliogharimu Sh350 milioni, jumba la kibiashara la Mamlaka ya Ustawi wa eneo la Ziwa, miongoni mwa miradi mingine.

Mnamo Mei 28, Rais Kenyatta atafungua rasmi Mbita Causeway.

Ataongoza sherehe za Madaraka Dei zitakazoandaliwa katika uwanja mpya wa michezo wa Jomo Kenyatta. Mnamo Jumatano, katibu wa usalama wa ndani Karanja Kibicho aliongoza kamati ya sherehe za kitaifa kuzuru uwanja huo kukagua hali yake. Kamati hiyo ilisema kwamba kazi husika itakamilika kwa wakati.

Akiongea na wanahabari baada ya ziara hiyo, Dkt Kibicho alieleza kwamba kwa sababu ya kanuni za kuzuia msambao wa corona, ni watu wachache watakaoruhusiwa ndani ya uwanja.

“Ni watu 3,000 pekee watakaoruhusiwa ndani ya uwanja wakati wa sherehe hizo huku wengine 20,000 wakifuatilia nje ya uwanja ambako kutawekwa runinga kubwa,” alisema.

Bw Kibicho alikuwa ameandamana na Gavana wa Kisumu Anyang’ Nyong’o na maafisa wengine wa serikali.

Kumekuwa na mabadiliko katika muundo wa uwanja huo ili uweze kusitiri watu wengi ikiwa ni pamoja na kupanuliwa kwa eneo la watu mashuhuri.

“Viwanja havijengwi ili kutumiwa kwa hafla kama hizi na kwa kawaida tungefanya upanuzi usio wa kudumu ili jukwaa la rais liweze kutoshea na kisha tulibomoe. Lakini kwa kuwa tuko na sehemu kubwa hapa tumeamua kujenga eneo la kudumu ambalo litasaidia kwa hafla nyingine siku zijazo,” alieleza Dkt Kibicho.

Kwa wiki kadhaa, jiji la Kisumu limekuwa na shughuli nyingi, huku barabara zinazoelekea katika uwanja huo zikikarabatiwa na kuwekwa alama.

Tayari, kazi ya ujenzi wa barabara ya kilomita 63 kutoka Mamboleo-Miwani-Chemelil itakayogharimu Sh4.9 bilioni imeanza.

Mwanakandarasi anayejenga barabara ya pande mbili ya Kisumu Boys-Mamboleo anajitahidi kumaliza kazi kwenye barabara hiyo ambayo itatumiwa na Rais na wageni wengine siku hiyo.

Barabara zinazoelekea uwanja huo tayari zimewekwa lami na taa za barabarani. Ikulu ndogo ya Kisumu pia inaendelea kufanyiwa mageuzi ikiwa ni pamoja na kuweka ua wa saruji.

Kuonekana kwa ndege za kijeshi katika anga ya kaunti hiyo zikifanya mazoezi ya sherehe hizo pia imefurahisha wakazi wengi.

Hata hivyo, haijabainika iwapo uwanja huo utatumiwa kwa mechi inayosubiriwa kwa hamu kati ya Gor Mahia na AFC Leopards alivyoahidi Rais Kenyatta kuashiria kufunguliwa rasmi.

You can share this post!

Wazee waingilia zogo la Matiang’i, Ongwae

Wadai taarifa ya pesa zilizotumika kwa BBI