• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 9:35 PM
CHOCHEO: Usimkaribie tu, mguseguse…

CHOCHEO: Usimkaribie tu, mguseguse…

Na BENSON MATHEKA

“SIO kwa ubaya lakini nimemchoka,” Carol aliambia wazazi wake walipomuuliza sababu ya kumwacha mumewe wa miaka mitatu. “Hanipi raha,” aliongeza na kuondoka kwenda kukutana na Dan, mpenzi wake mpya.

Kwake, Dan alikuwa akimfanyia anachohitaji kufurahia mapenzi. Alikuwa akimchangamkia na kumpapasa tofauti na mumewe ambaye alidai hakuwahi kumgusa isipokuwa wakati wa tendo la ndoa ambalo mwanadada huyo anasema hakulifurahia hata chembe.

Ikiwa Carol alichoshwa na mumewe baada ya miaka mitatu tu, sijui tusemeje kumhusu, Iba. Ni mwanamume mwenye umri wa miaka 35 aliyeteseka kwa miaka sita kabla ya kumtema mkewe. Iba anasema mkewe hakuwahi kumgusa hata siku moja.

“Hata tukiwa kitandani, tulikuwa sawa na milima miwili au pande mbili za sumaku zisokaribiana. Ile raha ambayo mwanamume hutarajia kupata kwa kuguswa na mpenzi wake haikuwepo. Nikijaribu kumgusa ilikuwa sawa na kushika mfu. Hakuhisi chochote na alikuwa na hasira mbaya,” asema.

Masaibu ya Carol na Iba ni sawa na yanayosababisha watu wengi kukosa raha ya ndoa. Wataalamu wa masuala ya mapenzi wanasema kuwa kugusa mpenzi wako kuna raha na faida ya kipekee inayokuza uhusiano. “Usipomgusa mpenzi wako na hasa yawe mazoea, utamkosesha raha na anaweza kukuacha. Hata kama hamtatengana, ataenda kutafuta raha kwingine,” asema Tito Umilyo, mwanasaikojia wa shirika la Ultimate Love jijjni Nairobi.

“Ikiwa hataki umguse au kukugusa, basi uhusiano wenu umo hatarini,” asema.

Kulingana na wataalamu, kukwepa mgusano ni mapuuza.

“Kupuuza mchumba ni moja ya sababu za kuvunjika kwa mahusiano. Kunachangiwa na mambo kadhaa ikiwemo ugomvi au kushindwa kutimiza mahitaji ya mwenzio kikamilifu. Pia, kunaweza kusababishwa na michepuko,” aeleza Tito.

Kukosa mgusano ni sawa na kukosa mapenzi kwa mwenzio, asema Frenz Kawira wa shirika la Love Care jijini Nairobi, mtu huwa anatoa ishara kwamba hana mapenzi kwake.

“Ninachojua kwa hakika ni kuwa mtu akikosa kumgusa mpenzi wake, huwa anajiweka katika hatari ya kuachwa. Kugusana kwa wachumba iwe ni kwa kutomasana, kupapasana, kudekezana na kupigana pambaja na mabusu, kunafanya uhusiano wao kuwa imara,” asema Kawira na kuongeza kuwa ni tendo linalohitaji ubunifu ili kuibua raha.

“Kitu kinachofifisha raha katika uhusiano ni mazoea. Kuwa mbunifu katika kila kitu unachofanya kujenga uhusiano wa kimapenzi na mtu wako hatakuchoka,” asema Kawira.

Tito anasema kugusa mchumba wako kunaonyesha kwamba unamthamini na kumtambua. “Ni kitendo kinachodhihirisha kuwa unamthamini mtu wako na pale mtu anapokataa kuguswa au kuchangamka mwenzake anapomgusa, huwa anaashiria kwamba hana hisia za mapenzi kwake,” aeleza.

Wataalamu wanasema kwamba mpenzi akikupuuza ukimgusa, huwa anaonyesha umuhimu wako kwake umeisha.

“Ni kitendo cha kuchochea mapenzi na kikikosekana au kisipokaribishwa, elewa mambo sio mazuri,” aeleza Tito.

Kawira asema kuwa kuna vitendo vya kugusana vinavyochangia kustawi kwa mahaba kwa wachumba.

“Kuna raha ya aina yake mwanadada kulala katika kifua cha mpenzi wake. Kuna raha mtu wako kukuvuta kifuani na kukumbatia na kuna raha ya kubebwa hadi kitandani,” asema Kawira.

Mshauri huyu asema kuwa wanaume hupenda kudekezwa, kupigwa mabusu na kukandwakandwa mwili. “Wanawake wanaotambua siri hii, hupagawisha watu wao, unaweza kuchota akili ya mwanamume kwa kumdekeza tu,”asema.

Aidha wataalamu wanakubaliana kuwa kugusana kunafaulu pale mawasiliano kati ya wachumba yako sawa.

“Mawasiliano yakiwa shwari, mili huwa inachangamkiana. Yakivurugika, ukimgusa mtu wako utakuwa ukijisumbua bure,” asema Tito.

You can share this post!

FUNGUKA: ‘Dume kivuruge namba wani…!’

Ruto aahidi kuepuka madeni akiwa rais