• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 3:04 PM
WAPWANI WAPIGWA DAFRAU

WAPWANI WAPIGWA DAFRAU

Na CHARLES LWANGA

MPANGO wa kuunda muungano wa Pwani kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2022, umechukua mkondo mpya baada ya kuibuka kuwa mashauriano yao yameingiliwa na vyama kutoka maeneo mengine ya nchi.

Taifa Leo imefahamu kuwa vigogo wa siasa kutoka nje ya Pwani hawataki Wapwani kuungana wenyewe, mbali vinataka waungane na vyama vyao.

Njama ya vyama vya kitaifa kuingilia mazungumzo ya kuunda chama cha Wapwani zilifichuka baada ya chama cha Kadu-Asili kutangaza kimejiondoa katika mazungumzo hayo wikendi kikidai hakuna hatua zinazopigwa.

Chama hicho ni kati ya vinne vya Pwani ambavyo vilitarajiwa kuunganishwa kwa madhumuni ya kuunda chama kimoja au muungano wa vyama utakaotambuliwa kuwa wa Pwani. Vyama vingine ni Umoja Summit, Shirikisho na Republican Congress Party.

Afisa wa ngazi ya juu katika mojawapo ya vyama hivyo, alifichua kwa Taifa Leo kuwa kuna vyama mashuhuri vya kitaifa ambavyo vimeanza kuingilia mazungumzo yao ili kuzuia kuungana kwa vyama asili vya Pwani.

Haikubainika mara moja ni vigogo gani wa kisiasa ambao wameingilia mazungumzo hayo, lakini baadhi wamekuwa wakionyesha nia ya kuthibiti siasa za Pwani kwa ajili ya kura za eneo hilo.

Vyama vya kitaifa ambavyo vimeonyesha nia kubwa ya kukita mizizi Pwani 2022 ni ODM kinachoongozwa na Raila Odinga, na United Democratic Alliance (UDA) kinachohusishwa na Naibu Rais William Ruto.

Vingine ni Wiper kinachoongozwa na Kalonzo Musyoka, Amani National Congress (ANC) ambacho kiongozi wake ni Musalia Mudavadi na KANU chake Seneta wa Baringo Gideon Moi.

Haya yanajiri wiki chache baada ya Gavana wa Kilifi, Amason Kingi, ambaye amekuwa akiongoza kampeni ya umoja wa Pwani, kusema kuwa huenda juhudi za kuleta umoja wa Wapwani zikasambaratika baada ya wanasiasa kadhaa wa ukanda huo kususia wito wake.

Baadhi ya wanasiasa waliojiondoa katika mipango hiyo wakishuku kuwa Bw Kingi ana nia fiche, madai ambayo amekuwa akiyapinga kila mara.

Juhudi za muungano huo zilianza kuyumbayumba mapema Aprili wakati Bw Kingi na Gavana Hassan Joho walipoanza kuvuta pande tofauti kwa kufanya mikutano miwili sambamba.

Bw Joho anasisitiza kuwa nia yake ni kuunganisha Pwani ndani ya ODM, Kingi anataka kubuniwa kwa chama kipywa ilhali Gavana Salim Mvurya wa Kwale anatarajia kunganisha eneo hilo nyuma ya Naibu Rais William Ruto.

Pigo lingine lilikuwa ni tofauti zilizoibuka kuhusu suala la vyama husika kuvunjwa ili kubuni chama kimoja.

Kinara wa Kadu-Asili, Bw Gerald Thoya alisema chama chake kiliamua kujiondoa katika mipango hiyo baada ya mazungumzo ya umoja wa vyama vya Pwani kukwama.

“Mazungumzo haya yamegonga mwamba kwa sababu hadi leo hatujaelewana na muda unayoyoma. Hatuwezi kuketi tukisubiri mpango ambao vyama vyote vinne vimekosa kuelewana kuuhusu,” akasema.

Hata hivyo, viongozi wa vyama vitatu vilivyosalia walisema mazungumzo yangali yanaendelea na wana matumaini kuwa yatazaa matunda.

Katibu Mkuu wa Chama cha Umoja Summit, Bi Naomi Cidi alisema dhana kuwa Wapwani hawawezi kujisimamia kisiasa wala kufanya uamuzi peke yao lazima ikabiliwe vilivyo.

“Hii ni dhana mbaya ambayo tunaipinga na hivi karibuni tutatangaza uamuzi wetu,” akasema Bi Cidi.

Katibu Mkuu wa Chama cha Republican Congress Party, Bw Ibrahim Khamisi aliwaomba wakazi wa Pwani wawe na subira mazungumzo yakiendelea.

Naye Bw Adam Mbeto, katibu mkuu wa Chama cha Shirikisho, alisema licha ya misukosuko, jambo la maana ni kuwa vyama vyote vinne vimekubalina kuhusu umoja wa Wapwani, na ana matumani kuwa watafaulu kuunganisha vyama hivyo vinne.

You can share this post!

Raila alakiwa kishujaa tayari kwa Madaraka

Uhuru na Raila wazindua miradi Nairobi na Kajiado