• Nairobi
  • Last Updated April 16th, 2024 10:55 AM
Wilbaro yazoa ufuasi Nyanza na Magharibi

Wilbaro yazoa ufuasi Nyanza na Magharibi

Na DERICK LUVEGA

CHAMA cha UDA kinachohusishwa na Naibu Rais, Dkt William Ruto jana kiliandaa mkutano na wanachama wake waliojisajili katika maeneo ya Nyanza na Magharibi mwa nchi.Maeneo hayo mawili ni ngome za kisiasa za Kinara wa ODM Raila Odinga na mwenzake wa ANC Musalia Mudavadi.

Mkutano huo uliongozwa na Mwenyekiti wake Johnstone Muthama, Katibu Mkuu Veronica Maina na aliyekuwa Seneta wa Kakamega Bonny Khalwale.Walikutana na viongozi ambao wangependa kutumia tiketi ya chama hicho kuwania vyeo mbalimbali Magharibi mwa nchi na Nyanza 2022.

Viongozi hao walitoka katika kaunti za Vihiga, Kakamega, Bungoma, Busia, Kisii na Nyamira.Mikutano kama hiyo pia inatarajiwa kuandaliwa katika maeneo ya Eldoret, Nakuru, Meru na Mombasa mnamo Juni 3.

Viongozi hao waliwataka Mabw Mudavadi na Kinara wa Ford Kenya Moses Wetang’ula wauze ajenda zao kitaifa badala ya kuchochea uhasama wa kikabila dhidi ya viongozi wanaomuunga mkono Dkt Ruto eneo hilo.

Pia walimtaka aliyekuwa Waziri wa Biashara wakati wa utawala wa Rais Mwai Kibaki, Dkt Mukhisa Kituyi aungane na vuguvugu la Hasla wakisema hana uungwaji mkono wowote wa kumwezesha kuwania Urais.

“Tunajua kuna wawaniaji wa kiti cha Urais kutoka eneo hili. Hata hivyo, hawasikiki zaidi ya hapa ndiyo maana wamekumbatia siasa za kikabila. Nawarai washiriki kampeni maeneo mengine badala ya kujikita katika kuwashutumu wawaniaji kutoka nje wanaokuja kusaka kura hapa,” akasema Dkt Khalwale.

Seneta huyo wa zamani wa Kakamega aliwataka wawaniaji hao wavumishe UDA mashinani, akitangaza kuwa atakitumia chama hicho kuwania kiti cha ugavana 2022.

Bw Muthama naye alipigia upato vuguvugu la Hasla akisema linawajumuisha watu wa matabaka yote na akawataka wamuunge mkono Dkt Ruto 2022.

“Hakuna chama chochote ambacho kimekutana na wagombeaji wanaotaka watumie kuwania viti mbalimbali hapa. Tutaelekea katika maeneo mengine kukutana na wanachama wetu nyanjani ili kuimarisha chama chetu,” akasema Bw Muthama.

Viongozi hao pia walimpongeza Jaji Mkuu mpya Martha Koome baada ya kuteuliwa na Rais Kenyatta wiki jana.Japo Mabw Mudavadi na Wetang’ula wapo ndani ya Muungano wa One Kenya Alliance, Dkt Kituyi bado hajatangaza chama atakachokitumia kuwania Urais 2022.

Muungano huo unatarajiwa kuwasilisha mwaniaji moja wa Urais 2022. Kwa sasa unasukumwa na ufanisi walioupata kwa kushinda viti vya ubunge vya Matungu, Kabuchai na Useneta wa Machakos.

Bw Mudavadi amekuwa akisaka uungwaji mkono kwa kuandaa mikutano katika eneo la Mlima Kenya pamoja na kaunti za Uasin Gishu na Kajiado.

You can share this post!

Wakereketwa wa BBI waomba kukubaliwa kucheza reggae

RAILA AWASAKA JOHO, MVURYA