• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 5:29 PM
IEBC yalaumu polisi kwa vurugu za chaguzi ndogo

IEBC yalaumu polisi kwa vurugu za chaguzi ndogo

Na WALTER MENYA

MWENYEKITI wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), Bw Wafula Chebukati amelaumu polisi kwa kushindwa kudumisha usalama wakati wa chaguzi ndogo za hivi majuzi zilizokumbwa na ghasia.

Haya yanajiri huku ikiibuka kuwa tume imewasilisha ripoti ya uchaguzi mdogo wa eneobunge la Juja kwa Afisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (ODPP), ikimlaumu Gavana wa Kiambu, Bw James Nyoro na Mwakilishi wa Kike wa Kaunti hiyo, Bi Gathoni Wamuchomba kwa uhalifu katika uchaguzi na kutaka washtakiwe.

Kwenye hotuba kali katika hafla iliyoandaliwa na Shirika la Elections Observation Group (ELOG) Ijumaa jioni, Bw Chebukati alitaja visa ambavyo maafisa wa polisi waliotumwa kudumisha usalama katika chaguzi ndogo za majuzi walikataa kutii maagizo ya maafisa wa tume, kuhamishwa kwa maafisa wakuu wa polisi siku chache kabla ya chaguzi hizo na kutotumwa kwa maafisa wa kutosha katika vituo vya kupigia kura.

Bw Chebukati alidai kwamba Inspekta Jenerali wa polisi, Bw Hillary Mutyambai, amekataa ombi la kukutana na tume kutafuta njia za kuzuia ghasia kwenye chaguzi ndogo zijazo.

“Moja ya changamoto kuu zinazokabili mfumo wa uchaguzi nchini Kenya ni ukosefu wa usalama wakati wa uchaguzi ambao umefanya ghasia kuongezeka ilivyoshuhudiwa kwenye chaguzi ndogo za majuzi. Hii ni kinyume cha msingi wa uchaguzi huru na wa haki ambao haufai kuwa na ghasia na vitisho kulingana na ibara ya 81(e)(ii). Swali ambalo tunafaa kupata majibu ni wapi au ni nani aliye na jukumu na wajibu wa kuzuia au kukabili ghasia na vitisho wakati wa uchaguzi,” alisema Bw Chebukati.

Hafla ya Elog iliandaliwa kukabidhi mamlaka kutoka kwa aliyekuwa mwenyekiti Bi Regina Opondo hadi kwa mwenyekiti mpya, Bi Anne Ireri.

Maafisa wa polisi wanaotumwa kudumisha usalama wakati wa uchaguzi huwa maafisa wa uchaguzi kulingana na sheria ya uchaguzi ya Kenya ya 2011.

Kama maafisa wa uchaguzi, sheria inawahitaji wafuate maagizo ya IEBC. Hata hivyo, Bw Chebukati alisema kwamba katika chaguzi ndogo za majuzi, tume ilishuhudia maafisa waliotumwa kudumisha usalama wakitazama ghasia zikiendelea katika vituo vya kupigia kura na kujumuisha matokeo.

Kulingana naye, maafisa hao walikataa kuchukua maagizo halali kutoka kwa tume watulize ghasia na pia walikataa kuchukua hatua kuzuia ghasia kutokea.

Chaguzi ndogo zilifanyika majuzi wadi za Ganda, Dabaso, London na Rurii na maeneo bunge ya Msambweni, Matungu, Kabuchai, Bonchari na Juja. Chaguzi hizi zote zikikumbwa na ghasia, kukamatwa kwa maajenti wa baadhi ya vyama vya kisiasa na madai ya hongo.

Kufuatia ghasia zilizotokea kwenye chaguzi ndogo za Bonchari na Juja, kiongozi wa chama cha ODM Raila Odinga alitoa taarifa akishutumu polisi na maafisa wa serikali ambao hakutaja majina kwa ghasia hizo.

“Tulichoshuhudia katika chaguzi ndogo za Bonchari na Juja ni matumizi mabaya ya nguvu za polisi na onyesho la kutenda makosa pasipo adhabu kulikotekelezwa na maafisa wakuu wa serikali wanaojitakia makuu na kujipiga vifua,” alisema Bw Odinga.

“Vikosi vya usalama ni vya kuhudumia watu na si kutekeleza maslahi ya wale wanaofanya majaribio ya kisiasa,” aliongeza Bw Odinga.

You can share this post!

Kampuni yagundua kiwango kikubwa cha dhahabu

Kiongozi wa wasiomtambua Mungu hatimaye aonekaniwa na Yesu...