• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 7:45 AM
Thiwasco yaweka mikakati ya uboreshaji wa huduma za maji safi

Thiwasco yaweka mikakati ya uboreshaji wa huduma za maji safi

Na LAWRENCE ONGARO

KAMPUNI ya maji ya Thika, maarufu kama Thiwasco, imepanga mikakati ya miaka 20 ijayo kwa lengo la kutosheleza wateja wake kwa kuhakikisha wanapata maji safi.

Mkurugenzi wa kampuni hiyo Bw Moses Kinya, alieleza kuwa ifikapo mwaka wa 2040 kampuni hiyo itakuwa ikisambaza kiwango cha ujazo lita 63 milioni kwa siku ikilinganishwa na lita 17 milioni ya maji inayosambaza kwa sasa kila siku.

Alifafanua kuwa mradi wa maji wa Karimenu ulioko Gatundu Kaskazini, unaoendelea kwa sasa, ukikamilika, basi wakazi wa Thika na vitongoji vyake wapatao laki nne watanufaika pakubwa.

Alitaja maeneo ya Witeithie, Gatuanyaga, Munyu, Githima, na Kiganjo kama maeneo yanayostahili kupokea maji kwa wingi kutokana na idadi kubwa ya wakazi.

“Tunataka kuhakikisha ya kwamba baada ya miaka mitano ijayo hakuna mkazi yeyote wa Thika na vitongoji vyake atakuwa na shida ya kupata maji safi katika makazi yake,” alisema Bw Kinya.

Aliyasema hayo mjini Thika mnamo Jumatano wiki jana katika hafla iliyohudhuriwa na washika dau tofauti kwa lengo la kujadiliana kuhusu usambazaji wa maji safi mjini Thika.

Alisema pia wamebuni mikakati mipya ya teknolojia kutoa huduma zao kwa wateja wao wote ili kurahisisha kazi zao.

Tayari kampuni hiyo pia imechimba visima kadha katika maeneo tofauti kama Kilimambogo, Gatuanyaga na Matathia sehemu za Thika Mashariki.

Vile vile shirika moja la kimataifa la kutoka Denmark, DANIDA, litafadhili kampuni ya Thiwasco, kwa kitita cha Sh11 bilioni ili kuinua sekta hiyo ya maji mjini Thika na vitingoji vyake. Bw Kinya alisema wakati mradi huo utakamilika, utaweza kusambaza maji lita 36 milioni kwa siku.

“Miaka miwili ijayo shida ya maji kwa wakazi wa Thika itakuwa ndoto kwani kampuni ya Thiwasco itakuwa imesambaza maji sehemu nyingi,” alisema Bw Kinya.

You can share this post!

Nafula aongoza Larissa kunyeshea Asteras AV 10-0 Ligi Kuu...

RIZIKI: Janga la Covid-19 halizimi shabaha yake kubuni...