• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
Boresha afya yako kwa kunywa maji fufutende

Boresha afya yako kwa kunywa maji fufutende

Na MARGARET MAINA

[email protected]

MAJI ya kunywa ni sehenu muhimu katika kuboresha afya zetu kama binadamu, haswa katika kuimarisha miili dhidi ya magonjwa mengi.

Maji ya ufufutende, badala ya maji baridi kama ilivyozoeleka kwa watu wengi, yana faida tele kwa miili yetu.

Maji ya ufufutende yana manufaa zaidi mwilini kuliko maji baridi. Maji ya ufufutende husaidia katika uyeyushaji wa chakula, na pia huzilinda figo pamoja na viungo mbalimbali mwilini.

Jambo muhimu la kuzingatia ni kutambua kuwa maji ya ufufutende si yale ya moto, kwani yakiwa ya moto sana huwa na madhara kwa ngozi nyembamba ya ndani ya mdomo, ikiwemo ulimi.

Tufahamu kuwa maji baridi ya kunywa hugandisha mafuta yaliyopo ndani ya miili yetu, ikiwemo kuufanya mwili kutumia nguvu ya ziada kuyapasha joto maji hayo kabla ya kutumika mwilini.

Hali hiyo inapoendelea kwa muda mrefu, huweza kusababisha shinikizo la damu, kwani hukwamisha mzunguko mnyoofu wa damu mwilini; na hivyo kusababisha magonjwa mengine mengi kuibuka.

Pia ni vyema kutumia maji ya uvuguvugu yaliyotiwa limao au ndimu, ili kupunguza ‘radicals’ ndani ya mwili na pia kuleta ladha katika maji yenyewe.

Pia ni vyema kunywa maji hayo vuguvugu kabla ya kifungua kinywa, ili kurahisisha mfumo wa mwili kwa siku nzima.

Faida za kunywa maji ya ufufutende

  • Yanasaidia kupunguza uzito

Kama unasumbuliwa na uzito wa mwili wako na ungependa kuupunguza, unashauriwa kunywa maji ya ufufutende, kwani huweza kuongeza joto la mwili na kuupatia mwili uwezo wa kuchoma lehemu kwa siku nzima.

  • Yanaboresha mzunguko wa damu mwilini

Mwili unapokuwa na limbikizo kubwa la mafuta (ambayo pia husababishwa na unywaji wa maji baridi), kinachotokea ni madhara mbalimbali katika afya yako.

Lakini unapotumia maji ya ufufutende, yanaenda kuyeyusha na kuondoa mwilini hiyo migando ya mafuta.

Hatua hii pia husaidia kuondoa sumu yote ndani ya mwili, na kuufanya mzunguko wa damu kuwa mzuri, ikiwemo kuwezesha misuli kupumzika.

  • Yanasaidia kuondoa mikunjo mwilini

Hakuna mtu anayependa kuzeeka mapema kabla ya wakati wake, hali ambayo mara nyingi husababishwa na uwepo wa “sumu” mbalimbali katika miili yetu.

Hata hivyo, unapokunywa maji ya uvuguvugu, husaidia kuondoa sumu hizo na kuusafisha kabisa mwili wako kwa ndani.

Maji hii yatasaidia kurejesha seli za ngozi yako, ili iwe na muonekano wa kuvutia na kuwa nyororo.

  • Kuondoa sumu mwilini

Faida nyingine ya kunywa maji ya uvuguvugu ni kutoa sumu zilizopo kwenye mishipa yako ya fahamu, na pia kuisadia figo yako kufanya kazi yake kikamilifu.

Hii ni tofauti kabisa na maji ya baridi, ambayo yanagandisha na kuilazimisha figo kuyeyusha kwanza maji hayo na kisha kuyachuja kabla ya kuyapitisha kutumika mwilini.

  • Kupata choo kwa urahisi

Maji ya ufufutende ni mazuri hata kwa kupata choo, kwa vile yanarahisisha uyeyushaji na uchambuaji wa kile kinachotakiwa na kisichotakiwa kutumika ndani ya mwili.

Faida nyingine ya kutumia maji ya ufufutende ni pamoja na kusafisha haja ndogo, na pia kuchangamsha utendaji kazi wa ubongo wako.

Aidha, kama uwezo wa kiuchumi unaruhusu, waweza kuyaongezea maji hayo limau na/au asali, kwani vitu hivyo si tu huongeza ladha, bali pia vina faida nyingi kiafya.

Fanya hivyo kila unapoamka asubuhi, kabla ya kula kitu chochote.

Kunywa maji ya ufufutende glasi mbili kisha kaa kwa muda wa saa moja hivi bila kula kitu ili kutoa nafasi kwa maji hayo kutumika mwilini kama ilivyoada.

Baada ya hapo, endelea kutumia vyakula vingine kama kawaida bila kusahau kufanya mazoezi ya viungo ili kuzidi kuboresha afya yako.

You can share this post!

RIZIKI: Janga la Covid-19 halizimi shabaha yake kubuni...

Duale apendekeza bunge litwikwe wajibu wa kuifanyia Katiba...