Na AYUMBA AYODI
Naibu rais mpya wa Shirikisho la Tenisi ya Mezani Afrika (ATTF) wa masuala ya maendeleo Mkenya Andrew Mudibo, ameahidi kufanyia mabadiliko miundo ya mchezo huo ili kufanikisha ukuaji wake barani humu.
Mudibo alisema msingi muhimu na nguvu za mchezo wowote zinatokana na maendeleo mashinani. “Tutaangazia kupanga upya miundo yetu ili iweze kuleta maendeleo katika mataifa 54 yanayojumuisha pia Kenya,” alisema Mudibo.
Rais huyo wa Shirikisho la Tenisi ya Mezani Kenya (KTTA) alichaguliwa bila kupingwa kuhudumu kama mmoja wa manaibu watano wa ATTF katika mkutano wa kila mwaka wa shirikisho hilo ulioandaliwa kupitia mtandao Jumamosi.
Khaled El-Salhy kutoka Misri alihifadhi urais wa ATTF kutumikia shirikisho hilo kwa muhula wa tatu naye Wahid Oshodi Enthan kutoka Nigeria ndiye naibu wake. Mudibo alisema kuwa watatafuta mbinu ya wachezaji wa Afrika kunufaika na udhamini na mashindano nje ya bara hili kupitia ushirikiano na mataifa yaliyoendelea katika mchezo huo.