Na MUTHONI KARIUKI
Kwa miaka minne sasa, Fridah amekuwa akimhakikishia Dan kwamba anampenda. Kama hawako pamoja, Fridah huwa anampigia simu na kumtumia jumbe za mapenzi kumhakikishia penzi lake kwake.
Lakini licha ya kumweleza kwa maneno na arafa za mapenzi, Dan anasema kwamba mwanadada huyu hajamuonyesha kwa vitendo kwamba anampenda.“Sijaona kitendo halisi kwamba ananipenda,” asema Dan na kutoa mfano alipougua kwa wiki tatu.
“Fridah hakunitembelea kamwe. Jumbe ziliadimika hadi aliposikia nimepata nafuu akaanza kunichangamkia tena. Ninahisi kwamba penzi la mwanadada huyu kwangu ni hewa tu. Maneno pekee hayatoshi, nataka mtu anayedhihirisha penzi kwa vitendo.
Sio mabusu na kulishana uroda pekee,” asema Dan.Kulingana na Dkt Catherine Keila, mtaalamu wa mahusiano ya mapenzi, maneno pekee na kulishana tunda sio dhihirisho kwamba mtu anakupenda.
“Maneno huchochea penzi. Lakini penzi la dhati ni vitendo, ni zaidi ya maneno matamu unayoambia au unayoambiwa na mtu. Kulishwa au kulishana uroda sio dhihirisho la mapenzi jinsi wanavyodhani baadhi ya watu,” asema Dkt Keila.
Mtaalamu huyu asema kuwa baadhi ya watu wanaopenda kutuma jumbe tamu za mapenzi hawawezi kudhihirisha penzi zaidi ya maneno yao.“Onyesha mtu wako kwamba unamjali na uchukue hatua kufanya hivyo kuliko maneno pekee.
Vitendo vya kujali hufanya mtu kuaminiwa zaidi. Ukimwepuka mtu wako akiwa katika shida au hali anayokuhitaji zaidi unamfanya akose imani nawe. Penda kwa vitendo, penzi bila vitendo ni hewa tu,” asema.
Wataalamu wanasema kwamba kitendo kikuu cha kuonyesha mapenzi ni kuheshimu mtu wako na sio kumlisha asali.“Muonyeshe heshima mkiwa pamoja au akiwa mbali. Zungumza mazuri ukiwa naye na ukiwa na wenzako,” aeleza Derick Mwachia wa shirika la Love Care, Nairobi.
Anasema vitendo kama kununulia mpenzi wako zawadi mara kwa mara ni muhimu katika kujenga penzi lakini hakiwezi kushinda heshima.“Saidia mtu wako kuwa bora zaidi, msaidie kujikuza na kujiendeleza kwa kila apendalo kufanya.
Ikiwa mpenzi wako anapenda soka, kuwa shabiki wake mkubwa na akiumia akicheza, mshughulikie uwezalo, usimtoroke hadi apone ili umchangamkie tena,” asema Mwachia.Dkt Keila na Mwachia wanakubaliana kwamba kitendo muhimu cha kudhihirisha mapenzi ni kuomba msamaha na kusamehe kwa dhati.
“Kuomba msamaha na kusamehe kwa dhati na kudhihirisha kwa kutokumbuka na kutotaja kosa hilo ni nguzo ya mapenzi. Inaonyesha utu ambao ukikosekana, uhusiano wowote wa mapenzi huwa balaa,” asema Dkt Keila.
Kitendo kikingine ambacho watu wanafaa kuzingatia ni kushirikisha wapenzi wao katika mipango yao, hasa waliooana.“Usipange mambo yako peke yako. Ni makosa kwa mke au mume wako kufahamu ulichukua mkopo unapolemewa kulipa.
Hii inayeyusha penzi lake kwako,” asema Mwachia.Kwa Dave Kimani, mpenzi wake wa miaka miwili alikuwa mtu wa siri nyingi ingawa alikuwa akimwambia kwamba alikuwa akimpenda.“Maneno yake yalikuwa matamu sana na alikuwa stadi wa kucheza ngoma chumbani.
Hata hivyo alikuwa mtu wa siri nyingi na hakuwahi kunionyesha kitendo kingine cha upendo isipokuwa kunilisha tunda. Nilimuacha na hakulalamika,” asema Kimani na kuongeza kuwa anaamini katika kuweka mipango pamoja na mpenzi wake.
Mwachia anasema vitendo kama kuwa karibu na mtu wako, kubadilishana maoni kuhusu mipango ya siku zijazo na kusaidiana katika mambo kadhaa ya furaha au huzuni vinachangia sana katika kujenga uhusiano wa kimapenzi.
“Watu hufurahishwa na mambo na vitendo tofauti. Chagua vitendo vinavyoonyesha mapenzi yako kwa mtu wako na utekeleze kimoja kila wakati,” asema.