• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Moto wateketeza nyumba zaidi ya 100

Moto wateketeza nyumba zaidi ya 100

Na SAMMY KIMATU

NAIROBI

FAMILIA zaidi ya 100 zimepoteza makazi baada ya moto mkubwa kuteketeza nyumba zao katika mtaa wa Kayaba, Kaunti ya Nairobi.

Wakazi wa eneo hilo waliambia Taifa Leo kuwa moto huo ulianzia ndani ya nyumba moja ambapo mwenyewe aliondoka na kusahau kuzima mtungi wa gesi ya kupikia.

“Kabla ya moto wa leo, usiku wa kuamkia leo majirani walizima moto mwingine kabla ya kuenea baada ya mtungi wa gesi kuwaka mkazi akiendelea na mapishi. Nimeweza kuondoa mitungi tano ya gesi wakati tukipambana kuuzima moto wa leo,’’ Bw Rodriques Lunalo, mkazi.

Fauka ya kuwa mkasa huo ulitokea wakazi wengi wakiwa kazini, Bw Lunalo aliwaongoza vijana kutoka mtaa wa Kayaba, Hazina na Sokoni kuungana pamoja kuzima moto.Kutokana na ukosefu wa barabara ya kuingia kwenye eneo la mkasa, vijana walilazimika kubomoa baadhi ya nyumba ili kuzuia moto kusambaa zaidi.

Wakati mmoja, vijana waliojawa na gadhabu ya gari la kuzimamoto kuingia mtaani, waliwarushia mawe maafisa wa kuzima moto kutoka serikali ya Kaunti ya Nairobi ndiposa wapore mali.Chifu wa Landi Mawe, Bw Mulandi Kikuvi alikikashifu kitendo cha vijana kupinga maafisa wa kaunti kuzima moto na kuongeza kwamba kitendo hicho kimepitwa na wakati.

“Nimethibitisha afisa mmoja wa kuzima moto amepigwa mawe na kujeruhiwa mguuni wake wa kushoto. Pia bomba la kupitisha maji ilikuwa imekatwa kwa panga ili maji yasifike kwenye eneo la mkasa,” chifu Mulandi akasema.

Kabla ya kuwasili kwa lori la kuzima moto, vijana walipanga foleni kuanzia mto Ngong hadi kwenye mkasa wakijihami kwa beseni na mitungi ya kuchota maji.Wengine nao walivunja paipu za kusambaza maji mtaani na kutumia maji yake kuzima moto.

Eneo la mkasa ilikuwa ni pahali palipojengwa nyumba za kukodisha na zilizokuwa zote zimejengwa kwa mabati.Vilevile, hakuna vibanda vya biashara vilyokuwa kwenye maeneo hayo.

  • Tags

You can share this post!

Afrika iongoze ukuzaji wa Kiswahili kimataifa

Shabana waomba uungwaji mkono