• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 5:29 PM
Leicester City kuvunja benki ili kumsajili Coutinho kutoka Barcelona

Leicester City kuvunja benki ili kumsajili Coutinho kutoka Barcelona

Na MASHIRIKA

LEICESTER City wako tayari kuweka mezani kima cha Sh6.4 bilioni ili kushawishi Barcelona kuwapa kiungo matata raia wa Brazil, Philippe Coutinho.

Coutinho, 29, aliingia katika sajili rasmi ya Barcelona mnamo Januari 2018 baada ya kuagana na Liverpool kwa kima cha Sh20 bilioni.

Liverpool tayari wamemweleza Coutinho kwamba hawapo tayari kuwania upya huduma zake muhula huu baada ya ajenti wa kiungo huyo, Kia Joorabchian kuulizia uwezekano wa kurejea kwa mteja wake ugani Anfield.

Coutinho ametatizika sana kufufua makali aliyokuwa akijivunia zamani uwanjani Anfield kabla ya kuyoyomea Uhispania kuvalia jezi za Barcelona mnamo Januari 2018.

Licha ya Barcelona kumshawishi Coutinho kuagana na Liverpool kwa mabilioni ya pesa, nyota huyo ameshindwa kusadikisha mashabiki wa miamba hao wa Uhispania kwamba alistahili kununuliwa kwa kiwango hicho cha fedha.

Kushindwa kwake kutamba ugani Camp Nou ni kiini cha Barcelona kumtuma kwa mkopo wa mwaka mmoja kambini mwa Bayern Munich mwanzoni mwa msimu wa 2019-20.

Japo ilitarajiwa kwamba Bayern wangalikuwa wepesi wa kumpokeza mkataba wa kudumu, mabingwa hao wa Ligi Kuu ya Ujerumani (Bundesliga) hawakuonyesha ari ya kuziwania huduma za Coutinho ambaye kwa sasa anamezewa pia na Inter Milan, Paris Saint-Germain (PSG), Juventus, Chelsea na Manchester United.

Kocha Carlo Ancelotti aliwahi pia kuwania maarifa ya Coutinho kabla ya kubanduka Everton na kurekea Uhispania kudhibiti mikoba ya Real Madrid.

Kwa mujibu wa Joorabchian, kubwa zaidi katika maazimio ya Coutinho ni kurejea Uingereza kuvalia jezi za kikosi chochote cha EPL iwapo Barcelona wataamua kumtia mnadani muhula huu.

Kocha Brendan Rodgers aliyemsajili Coutinho kambini mwa Liverpool yuko tayari kushawishi Leicester kufungulia mifereji yao ya fedha na kumsajili kiungo huyo.

Hadi alipobanduka ugani Anfield, Coutinho alikuwa ametawazwa Mchezaji Bora wa Mwaka kambini mwa Liverpool mara mbili na alikuwa amepachika wavuni zaidi ya mabao 50 katika kipindi cha misimu mitano.

Ujio wa kocha Jurgen Klopp uwanjani Anfield ulimkosesha Coutinho nafasi katika kikosi cha kwanza cha Liverpool. Hii ni baada ya mfumo mpya ulioletwa na Klopp kutowiana na mtindo wa kucheza kwa Coutinho.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Ukambani nao wafuata minofu Ikulu

Argentina na Chile waambulia sare ya 1-1 kwenye Copa America