• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 8:55 PM
Walevi Gatundu waasi pombe kujishughulisha na kazi za manufaa

Walevi Gatundu waasi pombe kujishughulisha na kazi za manufaa

Na LAWRENCE ONGARO

WALEVI katika kaunti ndogo ya Gatundu wameasi unywaji wa pombe haramu na kujihusisha na kazi za ujenzi wa taifa.

Vijana wapatao 16 waliozamia ulevi kwa muda mrefu kutoka kijiji cha Wamuguthuko na kile cha Kinyango walisema kuwa wamesitisha ulevi na kutaka kujihusisha na kazi za kuwanufaisha maishani.

Meneja wa NACADA katika Kaunti ya Kiambu Amos Warui, alieleza kuridhika kwake na hatua iliyochukuliwa na vijana hao.

Alieleza kuwa afisi yake itafuatilia mienendo ya vijana hao ili wasije wakarejelea uraibu wa kunywa pombe kupindukia.

Wakazi wa eneo hilo walifurahia hatua hiyo wakiitaja kama mwamko mpya.

Naibu Kamishna wa Gatundu Kusini Bw Stanely Kamande na Askofu wa Kanisa la Pentekosti Bw John Gichuhi, walipongeza hatua hiyo na kuitaja kama ya kipekee itakayoleta mabadiliko kwa vijana wengi eneo hilo.

Naibu Kamishna aliwaamuru machifu wawe macho mashinani kuona ya kwamba vijana hawapotelei kwenye unywaji wa pombe.

“Wazazi wengi wamefurahia hatua hiyo na bila shaka vijana hao wataanza maisha mapya ya kuboresha hali zao,” alifafanua Bw Kamande.

Aliwataka machifu wawe macho kuona ya kwamba vijana hawarejelei unywaji wa pombe haramu ambayo imeathiri maisha ya wengi vijijini.

“Wazazi wanastahili pia kuwa mstari wa mbele kuona ya kwamba vijana wote wanajishughulisha na mambo yatakayowanufaishga kimaisha. Nina imani wakazi wa eneo hili watakuwa raia wema na watakuwa mfano kwa maeneo mengine,” akasema.

Vijana hao waliahidiwa kupewa fedha za mikopo kupitia hazina ya Uwezo Fund ili waweze kujiendeleza na kufanya kazi za kujitegemea kama vile uchomeleaji wa vyuma, ujenzi, upakaji wa rangi, na hata uoshaji wa magari.

Vijana hao wamekiri ya kwamba uraibu wa kunywa pombe ulikuwa umewateka nyara, lakini wakasema kwa sasa wako tayari kujirekebisha.

You can share this post!

Mwatate, Bomet watoka sare 2-2

Raila akanyagia ‘tosha’ ya urithi wa Joho