• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 7:50 AM
Nassir na Shahbal walilia ‘tosha’ ya Raila uagavana Mombasa

Nassir na Shahbal walilia ‘tosha’ ya Raila uagavana Mombasa

VALENTINE OBARA na ANTHONY KITIMO

KIONGOZI wa Chama cha ODM, Bw Raila Odinga, alikwepa kumwidhinisha mwanasiasa yeyote kuwania ugavana Mombasa kupitia chama hicho mwaka ujao alipozuru kaunti hiyo.

Wanasiasa wawili wanaomezea mate tikiti ya chama hicho kuwania ugavana Mombasa mwaka ujao walionekana kuzidisha juhudi za kusaka ‘baraka’ za Bw Odinga.

Wawili hao ambao ni Mbunge wa Mvita Abdulswamad Nassir na mfanyabiashara Suleiman Shahbal, walionekana kung’ang’ania sikio la Bw Odinga alipozuru kaunti hiyo Alhamisi.

Bw Nassir na Bw Shahbal hawakukutana ana kwa ana hadharani katika hafla mbili ambazo Bw Odinga alihudhuria akiandamana na Gavana wa Mombasa, Bw Hassan Joho.

Hafla ya kwanza ambayo Bw Odinga alihudhuria ilikuwa ni uzinduzi wa kituo cha mafuta cha Hass katika mtaa wa Nyali, ambapo Bw Shahbal alikuwepo.

Baada ya kuandamana kwa karibu katika uzinduzi huo, wawili hao walienda kufanya mkutano wa faragha nyumbani kwa Bw Shahbal katika mtaa huo.

Ingawa waliyozungumzia hayakuanikwa wazi, duru ziliambia Taifa Leo kwamba, Bw Odinga alimwahidi Bw Shahbal kutakuwa na kura ya mchujo kwa njia ya haki na uwazi kuamua watakaopewa tikiti ya chama kuwania viti vyote vya kisiasa.

Baadaye, katika hafla ya kuzindua kitengo maalumu cha matibabu ya moyo katika Hospitali Kuu ya Rufaa ya Pwani, Bw Odinga alikumbwa na shinikizo kutoka kwa umati uliokuwa ukimrejeaja Bw Nassir kama ‘gavana mtarajiwa.’

Ingawa Bw Joho ndiye alikuwa mwandalizi wa hafla, Bw Nassir ndiye alitembea na waziri huyo mkuu wa zamani sako kwa bako walipowasili katika hafla hiyo. Bw Joho aliwafuata kwa karibu kutoka nyuma.

Katika hotuba yake, Bw Odinga alimtambua tu Bw Nassir kama mbunge mahiri ambaye amechangia mengi hasa katika wadhifa wake wa uenyekiti katika kamati ya bunge ya kuchunguza matumizi ya fedha za umma.

“Nataka kutoa shukrani kwa mbunge wa hapa kwa kazi anayofanya kufichua ufisadi katika bunge. Tunataka wabunge wetu waendelee kufanya kazi yao,” akasema Bw Odinga, huku mbunge huyo akisimama kando yake. Bw Nassir alisema kila mtu yuko huru kujiunga na ODM Mombasa lakini ana matumaini makubwa kwamba wapigakura watamchagua yeye kurithi kiti cha Bw Joho.

“Tumeona baadhi ya watu waliokuwa wakikashifu ODM katika uchaguzi uliopita wakirudi kutafuta kiti cha ugavana. wajue mimi ndiye nitakuwa gavana Mombasa” alisema Nassir.

You can share this post!

KENYA IMESOTA!

Vinara wa OKA sasa waalikwa kwa ndoa ya Uhuru na Raila