• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 3:04 PM
Mjukuu wa Moi asusia DNA, hatarini kushtakiwa

Mjukuu wa Moi asusia DNA, hatarini kushtakiwa

Na JOSEPH OPENDA

MJUKUU wake Rais (mstaafu) Marehemu Daniel arap Moi, anayeandamwa na kesi ya malezi ya watoto kutoka kwa aliyekuwa mkewe, huenda akashtakiwa kwa kutoheshimu amri ya mahakama.

Hii ni baada ya kukosa kujiwasilisha kufanyiwa uchunguzi wa DNA ilivyoamrishwa na mahakama moja ya Nakuru.

Bi Glady’s Jeruto Tagi, ambaye amemshtaki Bw Collins Toroitich, (pichani) sasa ametishia kuwasilisha kesi kortini. Katika maagizo ya korti yaliyotolewa Juni 16 na Hakimu Mkuu Mkazi Benjamin Limo, Bw Moi alihitajika kujiwasilisha katika Maabara za Lancet mnamo Ijumaa, Juni 18.

Chembechembe zake zilipaswa kutolewa ili kubaini ikiwa yeye ndiye baba mzazi wa watoto wawili waliohusishwa kwenye kesi hiyo.

Chembechembe hizo zingelinganishwa na zile ambazo zingetolewa kwa watoto hao wawili ambao amekanusha kuwazaa.

“Wahusika wameamrishwa kujiwasilisha (wakiandamana na wawakilishi wao mawakili) katika maabara za Lancet, Nakuru Juni 18, ili chembechembe zao zitolewe kwa uchunguzi,” Bw Limo aliamrisha.

Hata hivyo, Bi Jeruto kupitia wakili wake David Mong’eri alieleza Taifa Leo kuwa, Bw Moi hakujitokeza katika hospitali hiyo na pia hakuwasiliana kuhusu alipokuwepo.

“Wateja wangu walijitokeza hospitalini humo Ijumaa asubuhi na kukaa hadi adhuhuri lakini Bw Moi hakuja. Simu yake binafsi wala ya mawakili wake haikuwa ikiingia,” alisema Bw Mongeri.

You can share this post!

NI NCHI YA UNAFIKI

Spika Muturi awarai madaktari watumie teknolojia kwa tiba