• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 6:50 PM
Ndoa ya Jubilee na ODM yapigwa mawe

Ndoa ya Jubilee na ODM yapigwa mawe

Na BENSON MATHEKA

MUUNGANO unaosukwa wa vyama vya kisiasa vya Jubilee na ODM, unaendelea kukosolewa vikali huku viongozi walioalikwa kujiunga nao ukiiva wakisema, hauwezi kufaulu katika mazingira ya kisiasa nchini.

Mnamo Jumatano wiki jana, vyama hivyo vilitangaza kuwa vimeanza mazungumzo ya kuhalilisha ushirika ambao umedumu tangu handisheki kati ya Rais Uhuru Kenyatta na kiongozi wa chama cha ODM Raila Odinga Machi 9, 2018 kwa kuungana.

Kulingana na Katibu Mkuu wa Jubilee Raphael Tuju, vyama hivyo vinaunda muungano kwa msingi wa handisheki na vyama vingine vinaweza kujiunga baadaye bila mashartiHata hivyo, vinara wa vyama hivyo na washirika wao wamepuuza muungano huo wakiutaja kama mzaha na unaokiuka sheria.

Kulingana nao, lengo la muungano huo ni kumuandalia Bw Odinga njia ya kushinda urais mwaka ujao.Kiongozi wa chama cha Wiper Kalonzo Musyoka alisisitiza kuwa hawezi kushirikiana na Bw Odinga, waziri huyo mkuu akiwa mgombea urais.

Akizungumza akiwa Ithanga kaunti ya Murang’a Jumapili, Bw Musyoka alisema kwamba muungano wa ODM na Jubilee hautafua dafu.

“Tuko na mkataba wa ushirikiano kama Wiper na kiongozi wa Jubilee Party ambaye ni Rais Uhuru Kenyatta na mimi ndiye kiongozi wa chama cha Wiper na siwezi kuwa mgombea mwenza wa Bw Odinga,” alisema.

Mnamo Ijumaa, Naibu Rais William Ruto na washirika wake wa kisiasa walikejeli muungano huo wakiutaja kama wa kikabila.Dkt Ruto alisema muungano huo unalenga kuhujumu azima yake ya urais kupitia Jubilee Party lakini tayari amejipanga na chama cha United Democratic Alliance.

“Wanaweza kuunda muungano wa makabila lakini sisi tumejipanga katika chama cha hasla,” Dkt Ruto alisema akiwa kaunti ya Pokot Magharibi.

Alisema kwamba, Rais Kenyatta na Bw Odinga wanajisumbua bure kuunda muungano wa Jubilee na ODM.Wabunge wa vyama vya Wiper na Amani National Congress (ANC) wanasema kuwa muungano huo hautaweza kuvunja ule wa One Kenya Alliance (OKA).

“Jubilee na ODM wanaharibu wakati kwa kuwa muungano huo hautaenda popote. Ni njama ya kumcheza Odinga kwa kuwa ni wazi haungwi mkono Mlima Kenya,” alisema mbunge wa Lugari, Ayub Savula ambaye ni naibu kiongozi wa ANC.

Muungano wa OKA unaleta pamoja Bw Musyoka, Mudavadi, Moses Wetangula wa Ford Kenya na Gideon Moi wa KANU.Bw Musyoka Bw Mudavadi na Bw Wetangula ni washirika wa Bw Odinga katika muungano wa National Super Alliance (NASA) ambao wanasema ungali unadumu.

Bw Mudavadi na Bw Musyoka wamekataa mualiko wa kujiunga na ndoa ya Jubilee na ODM na kusisitiza wako OKA ambao kulingana nao, ni mkubwa kuliko wa vyama hivyo viwili.

Aliyekuwa Seneta wa Kakamega Boni Khalwale ambaye ni mshirika wa Dkt Ruto anasema itahitaji muujiza kwa muungano wa ODM na Jubilee kutikisa siasa Kenya.

“Unahitaji muujiza kwa sababu lengo ni kuafikia muungano wa kikabila,” alisema kwenye kipindi kimoja cha runinga jana asubuhi.

Kulingana na wabunge Dan Maanzo (Makueni na Chris Wamalwa (Kiminini) muungano unaosukwa katika ya ODM na Jubilee kwa sasa, unakiuka sheria kwa kuwa chama hicho cha chungwa kingali katika NASA.

“Vyama tanzu vya NASA haviwezi kuingia katika muungano mwingine lakini vinaweza kuwa na ushirikiano na vyama nje ya muungano huo,” walisema wakizungumza katika hafla tofauti.

You can share this post!

Argentina waangusha Paraguay huku Chile wakitoka nguvu sawa...

Peru wakung’uta Colombia huku Ecuador na Venezuela...