• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 11:14 AM
JAMVI: Madhara yanukia IEBC ikibanwa na muda wa maandalizi ya uchaguzi

JAMVI: Madhara yanukia IEBC ikibanwa na muda wa maandalizi ya uchaguzi

Na CHARLES WASONGA

TANGAZO la Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kwamba haitaweza kuweka mipaka mipya ya maeneo wakilishi kabla ya kufanyika kwa uchaguzi mkuu ujao, limeibua wasiwasi kuhusu kiwango cha utayari wa tume kwa uchaguzi mkuu ujao.

Licha ya mwenyekiti wa tume hiyo Wafula Chebukati kuwahakikishia maseneta kwamba ina uwezo wa kuendesha uchaguzi huo Agosti 9, 2022, inalalamikia uhaba wa fedha za kufadhili shughuli muhimu za maandalizi ya zoezi

.Kwa mfano, huku ikisalia miezi 13 pekee kabla ya Wakenya kuelekea debeni kuwachagua viongozi wapya, IEBC haijaanza shughuli ya usajili wa wapiga kura kwa wingi (mass voter registration.).

Aidha, haijanunua vifaa hitajika kwa uchaguzi huo kama mitambo ya kieletroniki (KIEMs kits) wala kuanza taratibu za utoaji zabuni ya uchapishaji wa karatasi za kupigia kura.

Kando na hayo, jopo la kuteua makamishna wapya wanne halijakamilisha shughuli hiyo huku nafasi ya Afisi Mkuu Mtendaji ikiwa ingali wazi tangu Ezra Chiloba alipopigwa kalamu mnamo Agosti 2019.

Hii ndio maana licha ya Bw Chebukati kuwahakikishia maseneta kwamba tume hiyo ina uwezo wa kuendesha uchaguzi wadadisi wanasema ina muda mfupi kuandaa zoezi hilo.

Kulingana nao, hali hii kwa kiwango fulani kimechangia na hatua ya serikali na wabunge kuelekeza juhudi zao katika masuala ya marekebisho ya katiba badala ya uchaguzi mkuu.

“Licha ya kwamba wanasiasa na serikali walifahamu fika kwamba tarehe ya uchaguzi mkuu ujao ni Agosti 9, 2022, kwa miaka mitatu iliyopita wanasiasa na maafisa wa serikali wamejikita zaidi katika mchakato wa BBI wala sio maandalizi ya uchaguzi. Kila mara, IEBC imekuwa ikilalamikia uhaba wa fedha za kuendesha shughuli zake lakini hakuna anayeshughulikia suala hilo,” asema Bw Felix Otieno, wakili na mtaalamu katika masuala ya uchaguzi.

Aidha, mtaalamu huyo anamlaumu Rais Uhuru Kenyatta kwa hali inayoikumba IEBC akisema kiongozi wa taifa alijivuta kutangaza wazi nafasi nne za makamishna waliojiuzulu mnamo 2018.

Wao ni aliyekuwa naibu mwenyekiti Connie Nkatha, Dkt Paul Kurgat na Margaret Mwachanya Wanjala pamoja na Dkt Roselyn Akombe aliyejiondoa kabla ya marudio ya uchaguzi wa urais mnamo Oktoba 26, 2017.

“Kujivuta huku kwa Rais Kenyatta kutangaza nafasi hizi kuwa wazi ndiko kulichangia IEBC kuendesha shughuli zake kwa karibu miaka mitatu ikiwa na makamishna watatu pekee. Wao ni mwenyekiti Bw Chebukati, Boya Molu na Profesa Abdi Guliye. Nadhani hii ndio maana tangu 2017 tume hii haijaendesha shughuli zozote za usajili wa wapiga kura ilivyofanya kabla ya uchaguzi wa 2017,” anasema Bw Otieno.

Kulingana na ripoti ya mwanasheria Johns Kriegler aliyechunguza kiini cha ghasia za baada ya uchaguzi mkuu wa 2007, muundo wa tume ya uchaguzi unapaswa kuwa mkamilifu miaka miwili kabla ya uchaguzi mkuu.

“Hii ndio itawezesha makamishna kupata uzoezi tosha wa kuendesha uchaguzi kwa njia ambayo itavutia imani ya washiriki wote. Bila kufanya hivyo, udhaifu fulani unaweza kutokea na hivyo kuibua hali ya sintoifahamu kuhusu uamunifu wa shughuli nzima ya uchaguzi,” ikasema ripoti hiyo iliyotolewa iliyokabidhiwa Rais mstaafu Mwai Kibaki mnamo Mei 15, 2008.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Kimataifa kuhusu Sera na Utatuzi Mizozo (ICPC) Ndung’u Wainaina anasema baadhi ya wanasiasa wameanza kuzungumzia uwezekano wa kuahirishwa kwa uchaguzi mkuu ujao kutokana na dhana kuwa IEBC haiko tayari kwa zoezi hilo.

“Huu ni unafiki mkubwa. Ni wanasiasa wawa hawa, ambao wamekuwa wakiendeleza siasa za BBI ambayo tayari imefyoza karibu Sh20 bilioni pesa za mlipa ushuru huku IEBC ikinywa fedha za maandalizi ya uchaguzi. Uchaguzi mkuu haowezi kuahirishwa isipokuwa ikiwa Kenya itavamiwa na taifa jirani,” anaeleza.

Kulingana na kipengele cha 102 (5) cha Katiba kipindi cha kuhudumu kwa bunge kinaweza tu kuongezwa ikiwa Kenya itakuwa ikishiriki vita na taifa jirani.

“Muhula bunge unaweza tu kuongezwa kwa miezi sita au muda usiozidi miezi 12 kupitia hoja itakayoungwa na angalau thuluthi mbili ya idadi jumla ya wabunge,” kipengele hicho kinasema.

Kikatiba, muhula wa bunge hufikia kikomo, wakati wa uchaguzi mkuu mwingine.Kutokana na hali hii, Bw Wainaina anaunga mkono pendekezo la Baraza la Maaskofu wa Kanisa Katoliki kwamba mchakato wa marekebisho ya Katiba kupitia Mswada wa Mpango wa Maridhiano (BBI) usitishwe ili juhudi zote zielekezwe katia maandalizi ya uchaguni mkuu ujao.

“Jopo la uteuzi wa makamishna wapya linaloongozwa na Bw Elizabeth Muli likamilisha shughuli hiyo haraka ili makamishna wanne wapya wateuliwe. Wadhifa wa Afisa Mkuu Mtendaji wa IEBC pia ujazwe na tume itengewe fedha zaidi za kufadhili maandalizi ya uchaguzi mkuu ili kuepusha ghasia zilizoshuhudiwa katika chaguzi za hapo nyuma,” anaeleza.

Itakumbukwa kwamba dosari katika sajili ya wapiga kura na utendakazi wa vifaa vya kielektroniki vilivyotumiwa katika uchaguzi mkuu wa 2017, ndio baadhi ya sababu zilizochangia kufutuliwa mbali kwa matokeo ya uchaguzi wa urais.

Hii ni kwa sababu, zabuni ya ununuzi wa vifaa hivyo ilitolewa kwa pupa, na pasina sheria kufuatwa, kwa sababu IEBC ilibanwa na wakati.Hii ni kwa sababu, mwenyekiti wa Bw Chebukati na wenzake sita, waliteuliwa Desemba 30, 2016 miezi minane kabla ya siku ya uchaguzi (8/8 2017).

Makamishna hao hawakuwa na muda tosha wa kujifahamisha na utendakazi wa asasi hiyo muhimu.Katika bajeti iliyosomwa bunge mwezi huu, Waziri wa Fedha Ukur Yatani aliitengea IEBC Sh15 bilioni za kufadhili maandalizi ya uchaguzi, fedha ambazo Bw Chebukati anasema ni finyu mnamo.

You can share this post!

Vinara wa NASA wawakanganya wafuasi wao

JAMVI: Nassir atagundua siri ya kurithi joho la...