• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 1:29 PM
Kiunjuri aonya Rais asijiongeze muda

Kiunjuri aonya Rais asijiongeze muda

Na STEVE NJUGUNA

KIONGOZI wa chama cha The Service Party (TSP) Mwangi Kiunjuri, amesema kwamba Rais Uhuru Kenyatta na serikali yake, wanafaa kuondoka mamlakani Agosti 2022.

Alisema kwamba chama chake kitaenda katika Mahakama ya Juu kutaka ushauri kuhusu mipango inayodaiwa kusukwa na serikali ya sasa ya kuongeza muhula wa Rais Kenyatta ofisini.

“Ni lazima waondoke ofisini Agosti 9 mwaka ujao, hakuna kuongeza muhula wa magavana, wabunge au Rais,” alisema.

Bw Kiunjuri alisema kwamba katika Mahakama ya Juu, chama chake kitaomba ufafanuzi kuhusu iwapo Mpango wa Maridhiano (BBI) unaweza kuwa sababu ya kuongeza muhula wa serikali iliyo mamlakani kwa wakati huu.

Alisema litakuwa jambo la busara kwa Rais kumaliza kipindi chake inavyosema katiba na kuondoka ofisini.

“Katiba iko wazi na hivi karibuni tutaelekea katika Mahakama ya Juu kutafuta ushauri kuhusiana na masuala ya kikatiba. Tutaomba Mahakama ya Juu itueleze mambo kadhaa na ushauri kuhusu iwapo BBI inaweza kuwa sababu nzuri ya kuongeza muda wa serikali hii,” alisema Bw Kiunjuri akiwa katika kijiji cha Limunga Kaunti-ndogo ya Laikipia Magharibi wakati wa mazishi ya Sophia Nyambura Kimani, mama wa diwani wa Wadi ya Marmanet, Simon Kanyutu.

Kauli yake ilijiri siku chache baada ya Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kusema kuwa inakabiliwa na changamoto nyingi kabla ya uchaguzi mkuu ujao.

IEBC ilitaja uhaba wa pesa, muda na vizingiti vya kisheria kama changamoto kuu zinazoikabili katika juhudi zake za kuandaa uchaguzi huru na wa haki.

Hasa, IEBC inasema kwamba kutotengewa pesa za kutosha kumeifanya ishindwe kuandaa mitambo yake ya kiteknolojia kwa wakati.

Bw Kiunjuri alikosoa Rais Kenyatta kwa kile alichotaja kama kutoyapa kipaumbele mambo muhimu.

“Kilicho muhimu ni kwa serikali kutoa pesa kwa wakati kwa serikali za kaunti ili magavana waweze kulipa wafanyabiashara na wakandarasi ili pesa ziingie katika mifuko yetu. Wafanyakazi wa serikali lazima walipwe kwa wakati ili waweze kulisha familia zao.

“Lakini serikali hii imewavunja moyo Wakenya, tumeona pesa zikitoka kwa IMF na wafadhili wengine lakini tunachofanya ni kujenga barabara huku watu wakikosa chakula,” aliongeza Bw Kiunjuri.

Kiongozi wa TSP alisema kwamba kuna masuala muhimu ambayo yanaendelea kuathiri vibaya Wakenya ambayo yanafaa kushughulikiwa kwa dharura.

You can share this post!

Wanafunzi 30 wapokea ufadhili kutoka kwa MKU

Ukambi: Wazazi wahimizwa wakumbatie chanjo