• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 8:55 PM
KINA CHA FIKRA: Kuteka watoto nyara ni unyama na hatari kwa usalama

KINA CHA FIKRA: Kuteka watoto nyara ni unyama na hatari kwa usalama

Na WALLAH BIN WALLAH

KILA kunapokucha kunakucha na kucha zake!

Siku hizi kila kunapokucha utasikia visa vya kuatua moyo na kuogofya kabisa kwamba mtoto wa fulani amepotea au watoto fulani wametekwa nyara!

Licha ya hayo, mara utasikia ati watekaji nyara wametuma arafa kwa wazazi kudai walipwe kitita kikubwa cha pesa wakati huu wa ukame wa kupata hela!

Msiba mkubwa zaidi ni kwamba pesa hizo za dhuluma zikichelewa kidogo tu kuwafikia hao maharamia, utasikia kwamba mtoto aliyetekwa nyara amechinjwa na kupatikana akiwa maiti!

Makubwa zaidi ni kwamba watoto wengine hupotea vivi hivi tu wanapotumwa na wazazi wao au wanapotoka nyumbani kuenda kucheza na wenzao bila kupatikana taarifa zozote kuhusu kupotea kwao! Halafu baada ya msako wa siku kadhaa ndipo mwili hupatikana ati mtoto alinyongwa au alichinjwa baada ya kutendewa unyama!!

Katika hali kama hii, tuseme nini? Kunani jamani? Usalama uko wapi? Wazazi roho mikononi!! Nao watoto vifo visogoni! Nani atakayemnusuru nani kutokana na jangamizi hili la watoto kutekwa nyara na kuuawa kinyama kwa kuchinjwa kama kuku?

Wazazi wafanyeje? Waache shughuli zao za kila siku za kuenda kutafuta riziki wakae na watoto wao majumbani?? Au watawafungia watoto ndani ya nyumba kama kuku wanavyofungiwa vizimbani? Ama waache kuwatuma watoto madukani? Au watoto waache kutoka majumbani kuenda kucheza na wenzao? Mbinu mwafaka wa kufumbua mafumbo haya na kuvitegua vitendawili hivi ni zipi? Ipi dawa mujarabu ya kuadua msiba na mizingile kama hii kuhusu maisha ya watoto wetu? Hali ni tete! Maisha ya wanetu yamo hatarini kila leo! Utekaji nyara ni hatari kubwa kwa usalama wa watoto wetu! Tufanyeje?

Kwa upande mwingine, tukichuja na kuchungulia, vyombo vya dola na asasi za usalama, kunani? Usalama wetu uko wapi? Enyi walinda usalama mliokabidhiwa dhima na dhamana za ulinzi, mnatuhakikishia nini kuhusu usalama wa raia, mwananchi na hasa hasa watoto hawa wanaotekwa nyara na kupatikana wamechinjwa? Mnasemaje wazalendo wenzangu walinda usalama? Walindwa wanaangamia na kuomboleza! Wanalia! Au ulinzi umegeuka ulizi? Chonde chonde jamani! Tafadhali! Tunaomba ulinzi na usalama ulio salama salmini!

Ndugu wapenzi, wakati mwingine mimi hutamani mwanadamu angejua wajibu wa kuwalea na kuwalinda watoto wao kama nyani ambao huwatunza kwa kuwabeba na kuwap akata watoto wao kila wakati! Lakini hapana! Binadamu tuna akili zaidi! Tuwalinde watoto wetu! Utekaji nyara ukomeshwe na ukome kabisaaa!!!

You can share this post!

NDIVYO SIVYO: Tofauti katika matumizi ya vikanushi...

KAULI YA MATUNDURA: Mashekhe wanachangia kudorora kwa...