• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 11:55 AM
Mawakili wakosoa hatua ya kushtaki rais

Mawakili wakosoa hatua ya kushtaki rais

Na RICHARD MUNGUTI

RAIS Uhuru Kenyatta, Jumatano aliiomba mahakama ya rufaa ibatilishe uamuzi wa majaji watano kwamba anaweza kushtakiwa akiwa afisini.

Kupitia kwa mawakili wake, Rais Kenyatta aliyekata rufaa kupinga marufuku ya BBI aliomba uamuzi kwamba anaweza kushtakiwa ufutiliwe mbali.

Majaji saba wa mahakama ya rufaa waliambiwa uamuzi Rais Kenyatta ashtakiwe unaweza kutifua vita, vurumai na umesababisha mtafaruku wa kikatiba.

Mawakili Waweru Gatonye, Mohammed Nyaoga na Kimani Kiragu walisema sheria inamlinda Rais dhidi ya kufunguliwa mashtaka akiwa afisini.

Mabw Gatonye, Nyaoga na Kiragu waliwaambia majaji saba wa mahakama ya rufaa kuwa, majaji hao watano wa mahakama kuu walikosea kisheria walipoamua Rais Kenyatta anaweza shtakiwa.

“Rais Kenyatta hakushiriki kwa njia yoyote ile katika kesi iliyowasilishwa katika mahakama kuu na walalamishi zaidi ya 70 waliopinga mchakato wa mageuzi ya katiba almaarufu BBI,” Bw Gatonye aliambia mahakama ya rufaa jana. Bw Gatonye alisema Majaji Joel Ngugi, George Odunga, Enoch Chacha Mwita , Jairus Ngaah na Teresia Matheka hawakumpa fursa Rais Kenyatta kujibu madai kuwa alichangia kuzinduliwa kwa mchakato wa mageuzi ya katiba.

“Rais Kenyatta alikejeliwa kimakosa na majaji hao watano bila ya kupewa fursa ya kujitetea,” alisema Bw Gatonye.

Bw Nyaoga alisema Rais Kenyatta yuko na haki ya kushiriki katika masuala ya mageuzi ya katiba kama mwananchi na wala sio kama Rais.

“Naomba hii mahakama ikumbuke kuwa mchakato wa mageuzi ya Katiba ni suala la kisiasa linalowahusu wananchi wote,” alisema Bw Nyaoga.

Alisema Rais Kenyatta akiwa kiongozi wa chama kinachotawala cha Jubilee, anaweza kushiriki katika suala lolote la kisiasa.

Majaji hao saba walielezwa kuwa kutatokea mtafaruku wa kikatiba ikiwa Rais atafunguliwa mashtaka kutokana na utekelezaji wa majukumu yake ya kikatiba.

Pia Mabw Nyaoga , Gatonye na Kiragu walisema majaji hao watano wa mahakama hawakufuata mwongozo uliotolewa na Mahakama ya Juu kwamba “ Rais analindwa na katiba kama mwananchi yoyote yule.”

You can share this post!

Leon Goretzka na Declan Rice kati ya wanasoka 5 wanaoviziwa...

Khan ajiondoa katika kesi ya Gicheru ICC