• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 7:55 AM
Ruto aahidi wapiga kura bondeni uhuru wa kuamua

Ruto aahidi wapiga kura bondeni uhuru wa kuamua

Na GEORGE SAYAGIE

NAIBU Rais William Ruto ameahidi wa wakazi wa kaunti za bondeni kwamba hataingilia uamuzi wao kuhusu viongozi watakaowachagua kuwania nyadhifa mbalimbali kwenye uchaguzi wa 2022.

Mapema wiki hii, Dkt Ruto aliwaahidi wakazi wa Kaunti ya Narok kwamba, licha ya kuwa mkazi wa Narok baada ya kununua ardhi katika eneo la Transmara Magharibi, hataingilia demokrasia yao kwa kuwachagulia kiongozi.

“Hakuna mtu anayepaswa kutoka nje na kuchagua au kuwalazimishia kiongozi kama wakazi wa Narok au katika sehemu zozote za taifa hili. Tumieni haki zenu kidemokrasia na kuchagua viongozi mnaotaka kwa nyadhifa tofauti 2022,” alisema Dkt Ruto.

Dkt Ruto amejitahidi kunasa tena eneo la Narok, ambalo Rais Uhuru Kenyatta alipoteza kwa kiongozi wa upinzani Raila Odinga katika chaguzi za 2013 na 2017.

Amezidisha shughuli za kisiasa katika kaunti za Narok na Kajiado katika wiki za hivi majuzi akinuia kudhibiti kisiasa jamii ya Wamaasai.

Naibu Rais tayari anakabiliwa na kitendawili kigumu kisiasa kwa sababu wandani wake kadhaa wanamezea mate viti vya ugavana katika eneo la Bonde la Ufa.

Kizungumkuti kinachomsubiri Dkt Ruto kinatokana na hali kwamba, idadi kubwa ya wagombea watawania tiketi ya chama chake cha United Democratic Alliance (UDA) na huenda wanategemea usaidizi wake kupata uteuzi kwa kinyang’anyiro hicho.

Tayari, makabiliano makali kisiasa yanatokota huku vikosi vya Naibu Rais vikijiandaa kuwabwaga viongozi wa kaunti hizo huku wengine wakijitayarisha kuwarithi wale waliokamilisha hatamu zao mbili za uongozi.

Kufikia sasa, wagombea wanaomezea mate tiketi ya (UDA) ili kutwaa kiti cha Gavana Samuel Tunai anayehudumu kipindi chake cha mwisho afisini ni wabunge watatu na waziri msaidizi mmoja.

Miongoni mwa vigogo walio mbioni kumrithi Gavana Tunai, ni Waziri Msaidizi katika Wizara ya Leba Patrick Ntutu na Mwakilishi Mwanamke Narok Soipan Tuya, wabunge Gabriel Tongoyo (Narok Magharibi), Korei ole Lemein (Narok Kusini).

Wengine ni Katibu wa Wizara ya Ugatuzi Charles Sunkuli, ambaye hajataja chama atakachokitumia kuwania kiti hicho.

You can share this post!

Nusu ya Wakenya hawajui chochote kuhusu BBI – Ripoti

BBI: LSK yadai ni rais alianzisha mageuzi