Na FARHIYA HUSSEIN
VIONGOZI wa dini ya Kiislamu kutoka Pwani wameikashifu Tume ya Kuajiri Walimu (TSC) kwa kutoa nafasi chache za walimu wa somo la dini hiyo (IRE).
Viongozi hao wamelalamika kuwa hali hiyo inazidi kusababisha uhaba wa walimu wa somo hilo hasa katika shule za umma na wakaipa TSC saa 72 kuongeza nafasi za walimu hao katika mpango wa kuajiri walimu.
“Kati ya nafasi zilizotolewa za kufundisha nchini na TSC, 12 tu ndio zimeeza kupeanwa kwa walimu wa IRE. Hiyo si haki,” alisema Mwenyekiti wa Baraza la Ushauri la Waislamu wa Kenya (Kemnac), Sheikh Juma Ngao.
Aliongeza kuwa wengi wa walimu hao hawana kazi na hulazimika kufunza masomo nyumbani ilhali wengi wao wamehitimu chuo kikuu.
“Tuna vyuo vikuu vya Kiislamu karibu kila eneo la nchi, lakini walimu hawa wanapohitimu huwa hawana mahali pa kufundisha,” alisema Sheikh Ngao.