• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 10:06 AM
CHOCHEO: Siri ya mapenzi yenye raha na yanayodumu

CHOCHEO: Siri ya mapenzi yenye raha na yanayodumu

Na BENSON MATHEKA

“Unajua ni kwa nini ndoa zinavunjika?” Sam Femi, mwanasaokolojia wa shirika la Dreams and Counseling Services, alimuuliza Peter* kwenye kikao cha ushauri nasaha.

Peter alijibu kwa haraka: “Ni kwa sababu ya wahusika kutowajibika.”

Lakini hilo sio jibu ambalo Sam alitaka japo alilitarajia. “Ni kweli, lakini ninataka kukueleza sababu ya kuvunjika kwa ndoa nyingi na kwa kiwango fulani uhusiano wa kimapenzi. Ni kwa sababu mmoja wa wahusika haongezi thamani kwa mwenzake,” Sam akasema huku akimtazama Peter usoni.

Baada ya kusita kwa sekunde kadhaa, Peter alizusha pumzi. “Ni kweli, umesema kweli,” akasema akionekana kama mtu aliyefunguka macho.

Kulingana na Sam, wengi huvutiwa kimapenzi na lakini hawaongezi thamani katika maisha ya wenzao.

“Uhusiano wa mapenzi ni zaidi ya urembo na kulishana asali. Kila mtu anatarajia mpenzi wake kuongeza thamani katika maisha yake. Hii inamaanisha kuwa mtu anatarajia zaidi ya kupashwa joto. Anataka uchangie kuimarisha uhusiano wake, wenu na maisha yake pia,” asema Sam.

Kulingana na mwanasaikolojia huyo, kuishi au kupenda mtu asiyeongeza thamani katika maisha yako, iwe kimawazo au kwa mali, ni kujibebesha mzigo mkubwa moyoni na mabegani.

“Ni kujilazimisha na hali ikiwa hivi, heshima ukosekana. Heshima ikikosa katika uhusiano wa kimapenzi, hauna budi kusambaratika kwa majuto,” alisema.

Kulingana na Dkt Eva Kamau wa shirika la Big Hearts jijini Nairobi, uhusiano unapokosa thamani huwa ni wa kulazimisha.

“Ukijilazimisha kwa mtu, hatakuheshimu. Badala ya kufanya hivyo, tafuta jinsi unavyoweza kuongeza thamani katika maisha yake na uhusiano wenu utanawiri na atakuheshimu,” asema Eva.

Mtaalamu huyu asema kwamba baadhi ya watu huwa wanasahau umuhimu wa kuongeza thamani baada ya kuolewa au kuoana.

“Hata baada ya ndoa, unafaa kuzidisha thamani yako kwa mchumba wako. Wanaojua siri hii wana raha katika ndoa lakini wanaopuuza hujuta,” asema.

Eva anafichulia wanawake siri rahisi sana ya kuongeza thamani kwa waume zao. “Ukiwa mtu wa kuongeza thamani kwa ndoa, utamdhibiti mtu wako. Hivi ndivyo, Rachael alifanya na akawa anamtawala Yakub hata kimawazo inavyoelezwa katika Bibilia. Rachael alikuwa mchapa kazi na hata alikutana na Yakub kisimani akinywesha maji mifugo wa babake,” aeleza Eva.

Sam anakosoa watu wanaodhani kupata watoto na mtu kunatosha kuwa thamani ya uhusiano wao. “Kupata watoto ni kitu kizuri lakini fanya zaidi kuongeza thamani kwa mpenzi wako. Usifikiri utaweza mtu kwa sababu ya watoto. Kuna wanawake na wanaume wanaolea watoto wao peke yao. Unaweza kuzalia au kuzalisha mtu watoto lakini iwapo hauongezi thamani katika maisha yake, siku moja atakuacha tu,” aeleza Sam.

Kulingana na wataalamu, wazazi wanafaa kuwafunza watoto wao jinsi ya kuongeza thamani kwa wachumba wao kupitia hulka zao.

“Watu wanaweza kurithisha watoto wao hulka hii iwapo wanaitekeleza wenyewe na kuwaandaa vyema. Unaweza kuandaa watoto wako kwa kuwa msitari wa mbele kuongeza thamani kwa mchumba wako na pia kuhakikisha kuwa wanajitegemea maishani kama vile kuwapa elimu nzuri. Kwa mfano, ukitaka binti yako aheshimiwe na mume wake, mpe elimu bora awe na matumaini katika maisha yake ya baadaye,” aeleza.

Eva anasema kwamba wanawake ambao hawajafunzwa kuongeza thamani katika uhusiano huwa wanatendwa hata na wafanyakazi wao wa nyumbani wanaowapokonya waume zao.

“Sababu za baadhi ya wanawake kupokonywa waume wao na vijakazi wenye bidii wasio na urembo kama wao ni kwa kuwa hawatekelezi mambo muhimu ya kuongeza thamani katika ndoa zao. Utawezaje kuruhusu mjakazi kuzoeana na mumeo?” ahoji Eva.

You can share this post!

FUNGUKA: ‘Najua mtasema ni wazimu…!’

Ukabila sumu ya chama cha Pwani