• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 7:55 PM
Mchakato kusaka Naibu Gavana wa Nairobi waanza

Mchakato kusaka Naibu Gavana wa Nairobi waanza

Na COLLINS OMULO

JUHUDI za kumtafuta yule atakayehudumu kama Naibu Gavana katika Kaunti ya Nairobi zinaendelea kushika kasi, huku Bi Ann Kananu akikaribia kuapishwa kama gavana wa tatu.

Chama cha Jubilee (JP) kimeandaa orodha ya watu wanane wanaotarajiwa kupewa nafasi hiyo.Mnamo Juni 24, Mahakama Kuu iliidhinisha mchakato wa uteuzi na upigaji msasa wa Bi Kananu kuwa halali, hali ambayo inatoa nafasi kwake kuapishwa rasmi kama gavana.

Uamuzi huo ambao uliotolewa na majaji watatu uliunga mkono kutolewa kwa Bw Mike Sonko kama gavana.

Mahakama pia ilifutilia mbali uwezekano wa kuandaliwa kwa uchaguzi mdogo kuwawezesha wenyeji kumchagua gavana mpya.

Muda wa siku kumi uliotolewa na mahakama kwa yeyote anayepinga uamuzi huo kuwasilisha rufaa unaisha Ijumaa hii.

Ingawa mawakili wa Bw Sonko walikuwa wameiomba mahakama kusimamisha utekelezaji wa uamuzi huo kwa siku 21 ili kuwasilisha rufaa, hawajaeleza chochote hadi sasa ikiwa watawasilisha rufaa hiyo.

Katibu Mkuu wa Jubilee, Bw Raphael Tuju, alisema kuwa chama hicho tayari kina orodha ya watu na kinangoja tu muda huo uishe.

“Orodha ya watu hao imekuwa tayari kwa muda mrefu. Tutakapomaliza taratibu za mahakama, tutafanya uamuzi,” akasema Bw Tuju.

Kulingana na Sheria ya Serikali za Kaunti ya 2017 iliyopitishwa na Bunge mwaka uliopita, magavana wanahitajika kuwateua manaibu wao katika muda wa siku 14.

Mwaka uliopita, watu tisa walijitokeza kuwania ugavana ijapokuwa uchaguzi mdogo haukufanyika kama ilivyotarajiwa.

Imeibuka miongoni mwao ni wale ambao huenda wakateuliwa kuhudumu katika nafasi hiyo.Wao ni mwanasiasa Peter Kenneth, Katibu Mkuu wa ODM Edwin Sifuna, mwenyekiti-mwenza wa Sekretariati kuhusu Mpango wa Maridhiano (BBI) Dennis Waweru, mfanyabiashara Agnes Kagure na aliyekuwa gavana wa Kiambu, William Kabogo.

Wengine ni Mkuu wa Kitengo cha Utekelezaji katika Ikulu (PDU) Nzioka Waita, Katibu wa Wizara ya Miundomsingi Charles Hinga, Katibu wa zamani katika Kaunti ya Nairobi Peter Kariuki na aliyekuwa Msajili katika Baraza la Jiji la Nairobi, Bw Philip Kisia.

Majina ya wakili Steve Ogolla na mfanyabiashara Fred Rabong’o pia yametajwa kuwa miongoni mwa watu hao.

Hata hivyo, Bw Tuju alikataa kutaja lolote kuhusu majina hayo. Badala yake, alisema orodha hiyo ni ndefu ambapo inawashirikisha watu kutoka vyama tofauti vya kisiasa.

Mnamo Januari, Mkurugenzi wa Chaguzi katika ODM, Bw Junet Mohamed, alisema huenda chama hicho kikajiondoa kwenye mkataba wake na Jubilee ikiwa hakitahakikishiwa kupata nafasi hiyo.

You can share this post!

Matiang’i aahidi kukomesha utekaji nyara nchini

“Wakenya” watakaokimbilia Amerika kwenye Olimpiki